KAULI MBIU YA SIKU YA UKIMWI DUNIANI:“TANZANIA BILA MAAMBUKIZI MAPYA YA VVU, VIFO VITOKANAVYO NA UKIMWI NA UBAGUZI NA UNYANYAPAA INAWEZEKANA”


 Siku ya UKIMWI Duniani iliasisiwa  rasmi na Shirika la Afya la Umoja wa Mataifa  (WHO) mwaka 1998 na imeendelea kuadhimishwa kila mwaka ifikapo Desemba mosi kwa uratibu wa Shirika la Umoja wa Mataifa la Kupambana na UKIMWI (UNAIDS).

  Maadhimisho haya hutoa fursa ya kutathmini hali halisi na mwelekeo wa udhibiti wa UKIMWI na vilevile kubaini changamoto, mafanikio na mikakati mbalimbali katika kupambana na janga hili.

  Siku hii pia hutoa nafasi ya kuwakumbuka wale wote waliopoteza maisha yao kutokana na janga la UKIMWI na kuwajali yatima waliotokana na janga hili. Katika ngazi ya kitaifa siku hii huadhimishwa kwa mzunguko katika mikoa yote ya Tanzania Bara na mwaka jana iliadhimishwa kitaifa mkoani Lindi.


  Mwaka huu Tume ya Kudhibiti UKIMWI Tanzania (TACAIDS) na Uongozi wa Mkoa wa Dar es Salaam wameratibu maadhimisho haya kitaifa kwa kushirikiana na wadau mbalimbali. Katika ngazi ya kitaifa mwaka huu maadhimisho haya yalianza kuanzia tarehe 25 Novemba 2013 na yanafikia kilele chake tarehe 1 Desemba 2013. 

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mheshimiwa Jakaya Mrisho Kikwete anatarajiwa kuwa Mgeni Rasmi kwenye kilele cha maadhimisho haya yatakayotanguliwa na matukio mbalimbali ikiwemo Maonyesho ya Shughuli za wadau wa udhibiti UKIMWI Nchini yaliyoanzakufanyika katika viwanja vya Mnazi Mmoja Mkoani Dar es Salaam kuanzia tarehe 25 Novemba 2013.

Vilevile katika maadhimisho hayo kulikuwepo  na kongamano la kitaifa la kutathmini hali na mwelekeo wa udhibiti UKIMWI nchini lililofanyika tarehe 27 na 28 Novemba 2013 kwenye Ukumbi wa Kimataifa wa Mwalimu Nyerere jijini Dar es Salaam.

Kauli mbiu ya maadhimisho ya mwaka huu inaendelea kuwa “TANZANIA BILA MAAMBUKIZI MAPYA YA VVU; VIFO VITOKANAVYO NA UKIMWI NA UNYANYAPAA INAWEZEKANA”. Kauli mbiu hii inalenga kutoa msukumo wa utekelezaji wa mikakati ya kudhibiti UKIMWI kitaifa na kimataifa ili kufikia azma ya sifuri tatu (3) yaani maambukizi mapya sifuri, vifo sifuri na unyanyapaa sifuri ifikapo mwaka 2015. Kauli mbiu hii inahimiza utekelezaji wa dhati wa Malengo ya Maendeleo ya Milenia (Millennium Development Goals-MDGs) na maazimio yaliyowekwa kwenye Mkutano Maalum wa Umoja wa Mataifa kuhusu UKIMWI uliofanyika mwaka 2001 Jijini New York, Marekani.

Hata hivyo wito umetolewa kwa wananchi katika ngazi mbalimbali ikiwa ni pamoja na sehemu za kazi, makanisani, misikitini, mashuleni, na katika jumuia zetu mbalimbali kuadhimisha siku hii kwa njia mbalimbali kama vile Makongamano, Kumbukumbu za Wapendwa wetu waliofariki kwa UKIMWI, Midahalo, Mikutano ya wazi, Vipindi kupitia vyombo vya habari, Kutembelea na kutoa misaada kwa yatima na wagonjwa wa UKIMWI, Kuzima mishumaa nk.

“TANZANIA BILA MAAMBUKIZI MAPYA YA VVU, VIFO VITOKANAVYO NA UKIMWI NA UBAGUZI NA UNYANYAPAA INAWEZEKANA”

Written by:Emanueli Onesmo Ndanshau
Posted by:http://www.info@dirayetu.blogspot.com

Share on Google Plus

About Unknown

This is a short description in the author block about the author. You edit it by entering text in the "Biographical Info" field in the user admin panel.
    Blogger Comment
    Facebook Comment

0 comments:

Post a Comment