Naibu katibu Mkuu CCM (Tanzania Bara)Mwigulu Mchemba amekwama kumzuia Dk. Slaa

NAIBU Katibu Mkuu (Tanzania Bara) wa Chama cha Mapinduzi (CCM), Mwigulu Mchemba, ameambulia patupu baada ya mikakati yake ya kutaka kukwamisha mkutano wa Katibu Mkuu wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA), Dk. Willibrod Slaa, kushindikana.
 
Tukio hilo lilitokea juzi jimboni Iramba Magharibi ambalo analiongoza Mwigulu, ambapo Dk. Slaa alifanikiwa kuwahutubia mamia ya wananchi katika mchakato wa chama hicho kukusanya maoni ya wafuasi wao juu ya rasimu ya kwanza ya Katiba mpya.
Kwa mujibu wa vyanzo vyetu vya habari, Mwigulu alijaribu kufanya kila mbinu ili mkutano wa Dk. Slaa ukose watu wa kumsikiliza lakini ilishindikana.
 
Tofauti na mikutano mingine ya CHADEMA ambayo ameihutubia Dk. Slaa katika mchakato huo, juzi hali ya ulinzi ilikuwa tofauti kidogo kutokana na polisi wengi kutanda eneo la mkutano la uwanja wa soko la zamani la Kiomboi wilayani Ilamba wakiwa na silaha za moto.
Askari hao ambao walikuwa wamezunguka eneo alilokuwa akihutubia Dk. Slaa, walivalia
kofia ngumu kama vile wanakwenda katika mapambano, jambo ambalo wananchi walidai kuwa ulikuwa ni mkakati wa kuwatisha wasijitokeze kumsikiliza kiongozi huyo.
Pamoja na jitihada hizo, wananchi walijitokeza kwa wingi kumsikiliza Dk. Slaa na kisha kutoa maoni yao kwa njia ya kujaza fomu na wengine kwa kuzungumza mkutanoni.
“Kusema ukweli usione tumejitokeza hapa ni kutokana na ujasiri wetu vinginevyo hali hii kwa wananchi wa kawaida lazima waogope maana askari hawa wanaonekana kama vile wamekuja kupambana,” alisema mmoja wa wakazi wa Kiomboi ambaye hakutaka jina lake litajwe.
 
Katika kuhakikisha wananchi hawahudhurii mkutano huo, siku moja kabla yalitolewa matangazo ya kuwaalika watu kwenye mashindano ya mpira wa miguu kati ya timu ya Kiomboi na Simba ya Dar es Salaam ambayo ililetwa na mbunge huyo, wakielezwa kuwa kiingilio ni bure.
 
Chanzo chetu kiliongeza kuwa baada ya viongozi wa CHADEMA kunasa mbinu hiyo, walijitahidi kuwaelimisha wananchi umuhimu wa kuhudhuria mkutano huo wa juzi, wakisema haukuwa wa siasa walizozizoea bali ni kuwataka watoe maoni yao juu ya rasimu ya Katiba mpya.
Akiwahutumia wananchi hao, Dk. Slaa alisema kuwa kuna vipengele vingi ambavyo wanaviunga mkono katika rasimu hiyo ingawa kuna baadhi vinahitaji marekebisho.
Alifafanua kuwa vipengele vingi ni vizuri japo CCM wanavipinga, huku akidai kwamba kitendo cha chama hicho tawala kupinga kipengele cha uwazi katika tunu za taifa pamoja na rushwa ni hatari katika taifa.
 
“Tunamuunga mkono Jaji Joseph Warioba katika vipengele vingi hasa katika kipengele cha kulinda rasilimali za taifa, uwazi katika mikataba lakini wenzetu wa CCM wamepinga kwamba uwazi usiwemo katika Katiba mpya sijui malengo yao nini. Kwa hiyo wananchi mnatakiwa kuamua wenyewe maana chama chenu hakitaki mambo mazuri yawekwe katika Katiba yenu,” alisema.
 
Naye mjumbe wa Kamati Kuu ya CHADEMA, Mabere Marando, alitoa ufafanuzi kuhusu mapendekezo ya serikali tatu ambazo alieleza kuwa CCM inapinga mapendekezo hayo.
Marando alisema kuwa kitendo cha baadhi ya wanasiasa wa CCM kuwapotosha wananchi kwamba serikali tatu ni mzigo kwa taifa si cha kweli na kwamba serikali ya sasa ndiyo mzigo kwa taifa.
 
“Kwa kuzingatia mapendekezo kuhusu Bunge la Jamhuri ya Muungano katika aya ya 105, kwa idadi ya sasa na mikoa ya Tanzania Bara na Zanzibar, Bunge la Jamhuri ya Muungano litakuwa na wabunge 75 tu.
“Kwa mapendekezo ya muundo wa serikali tatu, Bunge la Zanzibar litakuwa na wabunge 50 wa kuchaguliwa wakati Bunge la Tanganyika litakuwa na wabunge 189 wa majimbo ya uchaguzi,” alisema.
 
Marando aliongeza kuwa muundo wa muungano wa serikali tatu utakuwa na wabunge 314 tu; kwamba upo uwezekano wa idadi hiyo kupungua zaidi wakati wa mchakato wa kuandika Katiba ya Tanganyika na marekebisho ya Katiba ya Zanzibar.
Kuhusu Bunge la sasa ambalo linasemekana kuwa na unafuu, Marando alisema lina wabunge 357 ambapo 189 wanatokana na majimbo ya Tanzania Bara, majimbo 50 ya Zanzibar, Viti maalumu 105, kuteuliwa na rais 10, wanawakilisha watano wa Baraza la Wawakilishi Zanzibar na Mwanasheria Mkuu wa serikali.
 
Aliongeza kuwa kwa mabunge mawili  ya sasa yana idadi ya wabunge 438 na kwamba idadi hiyo ni kubwa kuliko idadi ya wabunge wa mabunge matatu yatakayokuwepo chini ya muundo wa serikali tatu.
Hata hivyo, baadhi ya wananchi waliopata fursa ya kuchangia walionekana kuchukizwa na madaraka makubwa ya Rais huku wakipendekeza kipengele cha kupunguza madaraka ya Rais kiingizwe kwenye Katiba.
Wananchi wengine walipendekeza Tume ya Taifa ya Uchaguzi iwe huru ili Rais asiweke mkono wake badala yake kiundwe chombo huru cha kuwachagua viongozi wa tume hiyo.
 
‘CCM imevunja Muungano’
Kutoka mkoani Kagera, mbunge wa Singida Mashariki, Tundu Lissu, amesema kuwa CCM tayari imeuvunja Muungano wa Tanganyika na Zanzibar, kutokana na muundo wa Katiba mbili za Muungano na ile ya Zanzibar.
Akiwahutubia wanachi waliohudhuria mikutano ya mabaraza ya wazi ya CHADEMA ya kujadili rasimu ya Katiba mpya mjini Bukoba, Lissu alisema kuwa Katiba hizo mbili zinaonyesha mkanganyiko wa wazi unaovunja Muungano.
Alisema kuwa Katiba ya Jamhuri ya Muungano inatamka wazi katika ibara yake ya kwanza kwamba Tanzania ni nchi moja ya Jamhuri ya Muungano, wakati ile ya Zanzibar nayo inatamka kuwa Zanzibar ni nchi, hivyo kuzifanya ziwe nchi mbili zenye madaraka kamili.
“Tanzania si nchi moja kwa mujibu wa Katiba ya Zanzibar, kwa sababu Muungano ulioasisiwa na Mwalimu Julius Nyerere na Sheikh Abeid Aman Karume, tayari umekufa na CCM ndiyo imeuua,” alisema.
 
Lissu alifafanua kuwa Zanzibar tayari ina alama zake ikiwemo wimbo wa taifa, rais wake ambaye ni mkuu wa vikosi vya idara maalumu, mahakama yake na bendera yake.
“Kuna haja sasa kufufuka Tanganyika kama Tume ya Jaji Warioba ilivyopendekeza kuwa na serikali tatu. Leo Jamhuri ya Watu wa Zanzibar imefufuliwa, kwa maana hiyo hakuna budi pia kufufuliwa kwa Jamhuri ya Tanganyika kutoka katika ‘wafu’,” alisema.
Share on Google Plus

About Unknown

This is a short description in the author block about the author. You edit it by entering text in the "Biographical Info" field in the user admin panel.
    Blogger Comment
    Facebook Comment

0 comments:

Post a Comment