MBUNGE wa Bukombe Profesa Kulikoyela Kahigi akataa takwimu za maji


MBUNGE wa Bukombe, Profesa Kulikoyela Kahigi (CHADEMA) amembana Naibu Waziri Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu, Tawala za Mikoa Serikali za Mitaa (Tamisemi), Aggrey Mwanri, aeleze takwimu za upatikanaji wa maji safi na salama kwa asilimia 52 amezipata wapi wakati shule nyingi za msingi, sekondari na vijiji hakuna maji.
 
Profesa Kahigi alitaka maelezo hayo jana bungeni alipokuwa akiuliza swali la nyongeza na kumtaka naibu waziri huyo aeleze ni jinsi gani amepata takwimu hizo wakati katika maeneo mengi ya wilaya ya Bukombe kuna uhaba mkubwa wa maji.
 
Aidha Mbunge huyo alitaka serikali ieleze ni lini miradi ya maji itakamilika katika mji mdogo wa Ushirombo na maeneo ya Iyovvu yaliyoko katika wilaya hiyo.
Awali katika swali la msingi la Profesa Kahigi, alitaka kujua serikali ina mkakati gani wa kuhakikisha wananchi wa Bukombe katika mji mdogo wa Ushirombo na vijiji vyake wanapata maji safi na salama katika kipindi cha miaka mitano.
Akijibu maswali hayo Mwanri alikiri kuwa wilaya hiyo inakabiliwa na tatizo la uhaba wa maji lakini takwimu alizopata zinatoka katika ofisi ya mkurugenzi wa halmashauri hiyo.
 
Mwanri alisema kuwa upatikanaji wa maji katika wilaya ya Bukombe na Mbogwe kwa wakazi 525,746 umefikia asilimia 52 kwa Julai, mwaka huu, huku asilimia 40 ilifikiwa Desemba mwaka 2012 kwa vijiji vya wilaya hiyo.
Alisema kuwa ongezeko hilo kwa kiasi kikubwa limechangiwa na utekelezaji wa program ya maji vijijini na usafi wa mazingira (RWSSP).
 
Aidha Mwanri alisema kuwa ifikapo Desemba 2013 inakadiriwa kuwa asilimia 60 ya wakazi wa maeneo ya vijiji watakuwa wanapata maji safi na salama chini ya program ya matokeo makubwa sasa (Big Results Now).
Mwanri alisema kuwa katika mwaka wa fedha 2013/14 wilaya hiyo imeidhinishiwa sh bilioni 1.083 kwa ajili ya kujenga na kukarabati miundombinu ya maji.
Share on Google Plus

About Unknown

This is a short description in the author block about the author. You edit it by entering text in the "Biographical Info" field in the user admin panel.
    Blogger Comment
    Facebook Comment

0 comments:

Post a Comment