Mamia ya wasafiri wa mikoani wakwama Dar.

  Walazimishwa kulipa nauli mara mbili
Mamia ya abiria wamekwama kusafiri kwa siku mbili katika Kituo Kikuu cha Mabasi yaendayo mikoani cha Ubungo (UBT), jijini Dar es Salaam

Waandishi wa NIPASHE Jumapili, waliofika kituoni hapo majira ya saa 2:00 asubuhi jana walikuta abiria wengi wakiwa wamekaa na mizigo yao na wengine wamesimama wakiwa wamekata tamaa baada ya kukosa usafiri wa kwenda mikoani na nje ya nchi.
Baadhi ya wasafiri walioongea na waandishi wa gazeti hili walisema, kwa siku mbili mfululizo hali ya huduma ya usafiri imekuwa mbaya na hakuna maelezo yoyote yanayotolewa.
Mabasi ambayo yanadaiwa kusitisha huduma zake ni yanayokwenda Dodoma, Tanga, Morogoro na nchi za jirani.
Walisema kinachofanyika kwa sasa, baadhi ya kampuni zinazoingiza magari machache kituoni hapo na kutoa huduma kwa masharti ya kulipa nauli mara mbili ya ile iliyoruhusiwa na serikali. Mmoja wa abiria aliyejitambulisha kwa jina la Pendo Makula, mkazi wa Dodoma, alisema alifika kituoni hapo jana alfajiri lakini mpaka muda huo alikuwa hajui hatma yake kutokana na kukosa usafiri.
Alisema, kulikuwa na taarifa zisizo rasmi kuwa magari mengi yamekodiwa na shule za sekondari na vyuo kwa ajili ya kusafirisha wanafunzi. Hata hivyo sababu hiyo haitoshi kuamini kwa sababu hiyo ni mara yao ya kwanza kushuhudia hali hiyo.
"Kama kweli magari yamekodiwa na wanafunzi, kwa nini wasiache mengine kutoa huduma kwa wananchi au kutoa matangazo ya tahadhari ili watu wasisumbuke?" alihoji Makula.
Abiria mwingine, Halima Jumatatu (18) ambaye ni mwanafunzi alisema alifika kituoni asubuhi na kukata tiketi kwa Sh.15,000 kwenda Tanga, badala ya nauli halali ya Sh. 13,000.
Hata hivyo, mpaka saa 4:00 asubuhi nauli ya kwenda Tanga iliongezeka na kufikia Sh.30,000, huku watu wanaokwenda Morogoro walikatiwa tiketi kwa Sh. 15,000 badala ya Sh. 7,000 na Dodoma ilikuwa Sh.30,000 badala ya Sh.16,000 hadi 18,000.
"Pamoja na kununua tiketi kwa bei ya juu, lakini basi tuliloambiwa tusafirie hatulioni, kila mtu anamuomba Mungu pengine tutapata usafiri leo," alisema Halima.
Raia mmoja wa China Tea Yu, alisema kwa siku mbili mfululizo alikuwa akikata tiketi ya kwenda Dodoma kwa matumaini ya kupata usafiri, lakini mpaka jana alikuwa kituoni hapo akisubiri bila mafanikio.
"Inatakiwa watu wafahamu muda ni mali, lazima tujali na kuthamini watu wanaopewa huduma, tumebaki hapa hatujui tufanye nini," aliongeza kusema Yu.
Kiongozi mmoja wa chama cha madereva ambaye hakutaka jina lake liandikwe gazetini, alisema tatizo kubwa ni upandaji wa nauli wa ghafla uliofanywa na wamiliki wa magari na kusababisha watu kushindwa kumudu viwango hivyo vya nauli.
Alisema kwa wale wenye uwezo wamelipa na wameondoka kwenye magari machache yaliyoonekana kituoni hapo.
"Kutokana na vyuo na shule kufunguliwa kuna wimbi kubwa la watu kusafiri, mabasi mengi yamepandisha nauli na unaowaona hapa ni watu masikini walioshindwa kulipa nauli inayotakiwa," alisema kiongozi huyo.
Katibu Mkuu wa Chama cha Wamiliki wa Mabasi nchini, (TABOA) Enea Mrutu, kwa kutumia ujumbe mfupi wa maneno (sms) kupitia simu ya kiganjani, alisema kutokana na shule na vyuo kufunguliwa jana na leo kutakuwa na shida ya usafiri. "Likizo zimekwisha shule zinafunguliwa, abiria ni wengi kwa leo na kesho na maonyesho ya biashara ya sabasaba ndio sababu ya abiria kukwama," ilisema ujumbe huo.
Afisa Uhusiano wa Mamlaka ya Udhibiti wa Usafiri wa Nchi Kavu na Majini (SUMATRA), David Mziray, alieleza kwamba hana taarifa ya kuwapo kwa tatizo hilo na kama litakuwapo basi litakuwa na mahusiano na ufunguaji muhula wa masomo katika shule mbalimbali nchini.
Hata hivyo, aliahidi kulifuatilia suala hilo, na kuwataka abiria waliokatiwa tiketi na kukosa usafiri kwenda kituo cha polisi kilichopo kituoni hapo kutoa taarifa.
SOURCE: NIPASHE JUMAPILI 

Share on Google Plus

About Unknown

This is a short description in the author block about the author. You edit it by entering text in the "Biographical Info" field in the user admin panel.
    Blogger Comment
    Facebook Comment

0 comments:

Post a Comment