MJUMBE "FEKI" KUKATWA MSHAHARA!!

Katibu wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania , Dk Thomas Kashililah 

Ofisi ya Bunge la Katiba, imemwandikia barua mwajiri wa Amina Mweta, ambaye alisaini posho ya Bunge hilo ili akatwe posho aliyoichukua katika mshahara wake.
Akizungumza na gazeti hili jana katika Ofisi za Bunge mjini hapa, Katibu wa Bunge la Jamhuri ya Muungano, Dk Thomas Kashililah, alisema Bunge limechukua hatua hiyo baada ya Mweta kuwajibu kuwa fedha walizompatia alikuwa ameshazitumia.
“Yeye (Amina Mweta), ni mwajiriwa wa Halmashauri ya Mwanga, tulichokifanya ni kumwandikia barua mwajiri wake ili akatwe katika mshahara wake,” alisema na kuongeza: “Atajua mwenyewe kama atalipa kwa kukatwa kidogo kidogo ama yote, lakini lazima ailipe posho hiyo aliyoichukua, kwa sababu alichukua na kuweka sahihi.”
Gazeti hili lilikuwa la kwanza kuripoti baada ya kutokea utata huo wa majina mawili ya wajumbe kufanana huku ikielezwa kuwa wote walikuwa wamesaini fomu za fedha za posho ya kujikimu ya Sh80,000 kwa siku kwa muda wa siku 13 unaomalizika Februari 28 mwaka huu ikiwa na maana kwamba kila mmoja alilipwa Sh1,040,000.
Mkurugenzi wa Shughuli za Bunge, John Joel, awali, alipoulizwa kuhusu utata huo alisema mjumbe halali ni yule aliyetoka Songea.
Hata hivyo, alisema kinachowashangaza ni kwamba yule mwenzake wa Mwanga alipotakiwa kurudisha fedha alizopewa kimakosa alisema ameshatumia sehemu kubwa na kubakiza Sh50,000 tu.
Akizungumza na gazeti hili, Mweta kutoka Mwanga alisema alipigiwa simu na Ofisi ya Bunge Maalumu la Katiba na kupongezwa kwa kuteuliwa na Rais kuwa mjumbe. “Mimi ni personal secretary (katibu muhtasi) wa Mkurugenzi wa Halmashauri ya Wilaya ya Mwanga na nilipigiwa simu na Ofisi ya Bunge wiki iliyopita nikipongezwa kwa uteuzi huo,” alisema.
Alisema alipofika na kujisajili baada ya kutoa kitambulisho chenye jina lake, alipewa kitambulisho na kisha kupewa malipo yake ya posho.
Naye Mweta kutoka Songea alisema alipigiwa simu na Katibu Mkuu wa COTWU kwamba aliteuliwa na Rais kuwa mjumbe na kutakiwa kuripoti bungeni.
Tayari Shirikisho la Vyama vya Wafanyakazi (Tucta) limeeleza kusikitishwa na utata wa watu hao wawili wenye majina yanayofanana kuwasili katika Bunge Maalumu la Katiba mjini Dodoma kwa nafasi ya ujumbe wa Bunge hilo, huku likisema halimfahamu Amina Mweta wa Kilimanjaro.
Katibu Mkuu wa Tucta, Nicholaus Mgaya mapema alikaririwa na gazeti hili akisema kuwa mazingira ya tukio hilo yamewatisha, hivyo kulazimika kumwandikia barua Katibu Mkuu Kiongozi, Balozi Ombeni Sefue ili kumthibitisha mjumbe wao halali. Chanzo;Mwananchi
Share on Google Plus

About Unknown

This is a short description in the author block about the author. You edit it by entering text in the "Biographical Info" field in the user admin panel.
    Blogger Comment
    Facebook Comment

0 comments:

Post a Comment