|  | 
| Katibu wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania , Dk Thomas Kashililah | 
Ofisi ya Bunge la Katiba, imemwandikia barua mwajiri wa Amina 
Mweta, ambaye alisaini posho ya Bunge hilo ili akatwe posho aliyoichukua
 katika mshahara wake.
                
              
Akizungumza na gazeti hili jana katika Ofisi za 
Bunge mjini hapa, Katibu wa Bunge la Jamhuri ya Muungano, Dk Thomas 
Kashililah, alisema Bunge limechukua hatua hiyo baada ya Mweta kuwajibu 
kuwa fedha walizompatia alikuwa ameshazitumia.
“Yeye (Amina Mweta), ni mwajiriwa wa Halmashauri 
ya Mwanga, tulichokifanya ni kumwandikia barua mwajiri wake ili akatwe 
katika mshahara wake,” alisema na kuongeza: “Atajua mwenyewe kama 
atalipa kwa kukatwa kidogo kidogo ama yote, lakini lazima ailipe posho 
hiyo aliyoichukua, kwa sababu alichukua na kuweka sahihi.”
Gazeti hili lilikuwa la kwanza kuripoti baada ya 
kutokea utata huo wa majina mawili ya wajumbe kufanana huku ikielezwa 
kuwa wote walikuwa wamesaini fomu za fedha za posho ya kujikimu ya 
Sh80,000 kwa siku kwa muda wa siku 13 unaomalizika Februari 28 mwaka huu
 ikiwa na maana kwamba kila mmoja alilipwa Sh1,040,000.
Mkurugenzi wa Shughuli za Bunge, John Joel, awali, alipoulizwa kuhusu utata huo alisema mjumbe halali ni yule aliyetoka Songea.
Hata hivyo, alisema kinachowashangaza ni kwamba 
yule mwenzake wa Mwanga alipotakiwa kurudisha fedha alizopewa kimakosa 
alisema ameshatumia sehemu kubwa na kubakiza Sh50,000 tu.
Akizungumza na gazeti hili, Mweta kutoka Mwanga 
alisema alipigiwa simu na Ofisi ya Bunge Maalumu la Katiba na kupongezwa
 kwa kuteuliwa na Rais kuwa mjumbe. “Mimi ni personal secretary (katibu 
muhtasi) wa Mkurugenzi wa Halmashauri ya Wilaya ya Mwanga na nilipigiwa 
simu na Ofisi ya Bunge wiki iliyopita nikipongezwa kwa uteuzi huo,” 
alisema.
Alisema alipofika na kujisajili baada ya kutoa 
kitambulisho chenye jina lake, alipewa kitambulisho na kisha kupewa 
malipo yake ya posho.
Naye Mweta kutoka Songea alisema alipigiwa simu na
 Katibu Mkuu wa COTWU kwamba aliteuliwa na Rais kuwa mjumbe na kutakiwa 
kuripoti bungeni.
Tayari Shirikisho la Vyama vya Wafanyakazi (Tucta)
 limeeleza kusikitishwa na utata wa watu hao wawili wenye majina 
yanayofanana kuwasili katika Bunge Maalumu la Katiba mjini Dodoma kwa 
nafasi ya ujumbe wa Bunge hilo, huku likisema halimfahamu Amina Mweta wa
 Kilimanjaro.
Katibu Mkuu wa Tucta, Nicholaus Mgaya mapema 
alikaririwa na gazeti hili akisema kuwa mazingira ya tukio hilo 
yamewatisha, hivyo kulazimika kumwandikia barua Katibu Mkuu Kiongozi, 
Balozi Ombeni Sefue ili kumthibitisha mjumbe wao halali.
Chanzo;Mwananchi 
0 comments:
Post a Comment