GHARAMA ZA SIMU: MJADALA MZITO WAIBUKA!!

Mkurugenzi Mtendaji wa Vodacom Tanzania Rene Meza, akizungumza na waandishi wa habari Dar es Salaam jana, kuhusu mwenendo wa kibiashara wa kampuni hiyo.
Wakati Mamlaka ya Mawasiliano Tanzania (TCRA) imeziagiza kampuni za simu kutoa maelezo kuhusu mabadiliko ya gharama za vifurushi vya muda wa maongezi, Vodacom Tanzania imeeleza kuwa mabadiliko hayo yanatokana na ongezeko la kodi na hivyo kulazimika “kubadili mazingira ya kibiashara ili kuepuka hasara”.
 
Kampuni nyingine kubwa ya mawasiliano, Tigo imeahidi kutoa ufafanuzi wa suala hilo kesho wakati Airtel imesema haijafanya mabadiliko yoyote kwenye gharama za vifurushi vyake.
Kumekuwapo na mijadala mingi katika mitandao ya kijamii kupinga bei mpya za vifurushi hivyo ambazo zimeelezwa kuwa ni megabati nane kwa vifurushi vyote vya saa 24, na megabati 60 kwa vifurushi vya wiki.
Bei hizo zinaelezwa kuwa zimeanza kutumika kwa wateja wanaotumia mitandao ya kampuni za Vodacom na Tigo, ambazo zinachuana vikali sokoni, huku baadhi ya wateja wa kampuni ambazo hazifanya mabadiliko ya gharama hizo wakiwashiwishi wenzao kuhama ili kutokuwa hewani kutokana na kukosa vifurushi.
Mkurugenzi Mkuu wa TCRA, Profesa John Nkoma alisema kuwa tayari mazungumzo kati ya mamlaka yake na kampuni hizo za mawasiliano yameshafanyika na kilichobaki ni wao kutoa maelezo ya hatua walizoichukua.
“Matumizi ya intaneti yameongezeka nchini na wananchi wengi wamekuwa hawajui namna ya kutofautisha vifurushi vya muda wa maongezi na vile vya intaneti. Lakini nimezungumza na kampuni zote na tumefikia mwafaka. Ndani ya wiki hii watatoa tamko lao pamoja na msimamo wa bei za vifurushi,” alisema Profesa Nkoma.
Machi, 2013, Profesa Nkoma alisema angehakikisha kampuni za simu zinawasilisha kwake makubaliano kuhusu punguzo la gharama za kupiga simu kwa mwingiliano wa mawasiliano, kutoka wateja wa kampuni moja kwenda nyingine.
Mabadiliko ya gharama na ukubwa wa vifurushi yalianza kujitokeza mwishoni mwa wiki iliyopita, hali iliyoibua mijadala mingi katika mitandao ya kijamii. Kilichojitokeza ni kwamba makampuni hayo yamepunguza ukubwa wa vifurushi vya intaneti na kutoathiri vile vya muda wa maongezi na ujumbe mfupi hali, iliyozusha hamaki kwa wateja wengi wanaotaka kujua sababu za mabadiliko hayo.
Baada ya mijadala hiyo kuongezeka, Naibu Waziri wa Sayansi na Teknolojia, January Makamba aliwaondoa wasiwasi wateja baada ya kuandika katika ukurasa wake wa facebook kuwa serikali imechukua hatua mara moja.
“Nimeongea na Mkurugenzi Mkuu wa TCRA, Profesa John Nkoma na nimemuagiza azungumze na kampuni za simu juu ya mabadiliko ya bei za bundles (vifurushi): ukubwa, ughafla na upamoja (mitandao yote). Nimewaagiza pia watoe majibu kwa umma haraka iwezekanavyo. Kampuni za simu hazipaswi kupanga au kuratibu kwa pamoja bei; tukigundua hilo limetokea ni ukiukwaji wa kanuni za ushindani wa soko,” inasema sehemu ya ujumbe huo.
Katika ujumbe wake, Makamba anafafanua kuwa Sheria ya udhibiti wa mawasiliano haiipi serikali nguvu ya kupanga bei, isipokuwa gharama za muingiliano
“Inawezekana gharama za uendeshaji, ikiwamo umeme, zinapanda, lakini hakuna kodi mpya ya Serikali tangu baada ya bajeti.

 Huko nyuma ushindani ulishusha bei kwa sababu hakukuwa na bei elekezi. Bado niko nje ya nchi kwa safari ya kiserikali, lakini nimekuwa nalifuatilia suala hili kwa karibu. Pia nimeongea na Mkurugenzi Mkuu wa Vodacom, Rene Meza, kuhusu suala hili leo asubuhi,” aliandika Makamba.


Mkurugenzi huyo wa Vodacom alisema ongezeko la bei za kupiga simu na kupungua kwa ukubwa wa vifurushi limesababishwa na ongezeko la kodi hivyo mabadiliko hayo yamefanywa kama hatua ya kubadili mazingira ya kibiashara ili kuepuka hasara.
“Tunafanya hivi ili tusipate hasara na tuendelee kuwekeza, kodi ni kubwa na lazima tufanye kila tuwezalo ili na sisi tuendelee kufanya kazi kwa faida,” alisema Meza.
Meza alisema hata hivyo kampuni ya Vodacom imepunguza viwango vya malipo vya upigaji simu ambapo mwaka 2013 dakika 1 ilitozwa Sh58 wakati hivi sasa dakika 1 inatozwa Sh24. Akaongeza kuwa bei hizo zimeshuka hata kwa vifurushi na kutoa mfano kuwa mwaka 2013 mteja alitozwa Sh9 kwa MB 1 na mwaka huu mteja anatozwa Sh5 kwa MB 1.
“Hili punguzo la bei ni kubwa na linatuumiza kwa sababu kodi zinakwenda juu, sisi tukishusha gharama lakini kodi zinaendelea kupanda. Kwa mfano mwaka 2012 kodi ilikuwa asilimia 5 na mwaka huu kodi imepanda hadi kufikia asilimia 79,” alisema.
Ofisa Uhusiano wa Kampuni ya Airtel, Jackson Mbando alisema kampuni yake haijabadili chochote katika muda wa maongezi wala katika vifurushi vya intaneti badala yake alisema Airtel imekuwa ikitoza gharama nafuu kuliko mitandao yote.
“Sisi tunatoa kila kitu kwa bei nafuu, kama kuna kampuni zinazoongeza gharama, hao waulizwe. Hapa kila kitu unapata zaidi,” alisema.
Hata hivyo, Mbando alisema hata kama kuna ongezeko, kampuni yake inatoza gharama nafuu za vifurushi vya intaneti kuliko kampuni nyingine za simu nchini.
Meneja Mawasiliano wa Tigo, John Wanyancha alisema amepata malalamiko hayo na kuahidi kuyatolea ufafanuzi mapema.
Wateja wengi wa kampuni hizo walilalamika kuwa wakiweka fedha kwenye akaunti zao wakati mwingine salio huisha hata kabla ya kupiga simu au kujiunga na kifurushi.
Mmoja wa wateja wa kampuni hizo alilalamika kwenye mtandao wa kijamii kuwa gharama hizo zimepanda kwa kuwa wananchi hawana pa kukimbilia.
“Sasa hivi mwisho kutuma video za kilobaiti mbili ili kuepuka kuwa nje ya mtandao baada ya kumaliza vifurushi vyetu. Wanajua hatuna pa kukimbilia ndiyo maana wameamua kutufanyia hivi,” aliandika mteja huyo katika akaunti yake ya WhatsApp.
Wengi wanalalamika kuwa vifurushi hivyo havikidhi mahitaji wala kuendana na thamani ya fedha wanazotumia. Mabadiliko haya yanakuja ikiwa ni baada ya Mamlaka ya Udhibiti wa Nishati na Maji (Ewura) kushusha gharama za umeme kwa shilingi nane kwa kila uniti moja agizo linaloanza kutekelezwa kuanzia jana.

 Wateja wengi wa Kampuni ya Tigo walilalamika kuwa wakijiunga na kifurushi cha muda wa maongezi, kwa mfano cha Minikabang cha Sh649 wanapata dakika 11 wakati zamani walipata dakika 14.

“Nashangaa siku hizi nakatwa Sh649, napata dakika 11 tu, halafu sielewi zinaishaje ishaje yaani nikipigia watu wawili, watatu, kifurushi kimeisha,” alisema, Pendo Malya, mkazi wa Tabata.
Kadhalika wateja wa mitandao ya Airtel na Vodacom nao walilalamika kukatwa fedha nyingi katika muda wa maongezi licha ya kampuni hizo kutangaza kuwa zimepunguza gharama.
Abdul Mfinanga, mkazi wa Msasani alisema anakatwa fedha nyingi hata wakati wa kufanya miamala katika huduma ya MPESA.
Asilimia kubwa ya wateja wa simu za mitandao yote walikiri kupaa kwa gharama za kupiga simu bila ya kujiunga na vifurushi.
Kwa mfano, Anuciata Mwigalula, wa Kibamba alisema akijiunga na muda wa maongezi anapata unafuu kidogo lakini akiweka Sh500 bila kujiunga, basi hawezi kuzungumza hata kwa dakika tatu hata akipiga kwenda mtandao ule ule.
“Wanatuibia sana, wakati mwingine unapewa ofa ya kuanzia saa sita usiku, sasa ukeshe ndiyo unufaike na huduma hizo?” alihoji Mwigalula.
Hata hivyo, Novemba mwaka jana, Makamba alikiri mbele ya Bunge kuwa kuna tatizo katika kampuni za simu nchini la kuwaibia wateja wao.
Share on Google Plus

About Unknown

This is a short description in the author block about the author. You edit it by entering text in the "Biographical Info" field in the user admin panel.
    Blogger Comment
    Facebook Comment

0 comments:

Post a Comment