BARAZA la Maadili ya Utumishi wa Umma limesikiliza shauri la mgawo wa
 fedha za Escrow dhidi ya aliyekuwa Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo
 ya Makazi, Profesa Anna Tibaijuka, ambaye anadaiwa amekiuka Sheria ya 
Maadili ya Utumishi wa Umma namba 12 (e) (1) ya mwaka 1995.
Kutokana na madai hayo, waziri huyo wa zamani wa Serikali ya awamu ya 
nne, amefichua namna alivyotumia fedha za mgawo wa Escrow ikiwamo 
kutumia Sh milioni 10 kwa ajili ya kununua mboga.
Profesa Tibaijuka alifikishwa mbele ya Baraza la Maadili jana jijini Dar
 es Salaam, na kusomewa mashtaka dhidi yake na Mwanasheria wa baraza 
hilo, Wema Winfred.
Mwanasheria huyo, alidai kuwa Profesa Tibaijuka anakabiliwa na mashtaka 
matatu, ambayo ni kuomba fadhila za kiuchumi kinyume na sheria ya 
maadili kifungu namba 6, kupokea fadhila za kiuchumi kinyume na sheria 
hiyo na kuwa na mgogoro wa kimasilahi.
Alidai kuwa mshtakiwa huyo alikiuka maadili ya umma kwa kuomba 
kuingiziwa fedha kiasi cha Sh bilioni 1.6 kutoka katika Kampuni ya VIP 
Engineering and Marketing Tanzania Limited ambazo aliingiziwa kwenye 
akaunti namba 001200102640201 iliyopo Benki ya Mkombozi, Tawi la St. 
Joseph jijini Dar es Salaam.
Mwanasheria huyo alidai kuwa mshtakiwa kwa kutumia wadhifa wake, 
alijinufaisha kifedha, hivyo baraza linamtaka kueleza bayana mwenendo 
wake kabla ya hatua zaidi za kisheria hazijachukuliwa dhidi yake.
Baada ya kusomewa mashtaka hayo, mbele ya baraza hilo, alisimama 
mwanasheria wa Profesa Tibaijuka aliyejitambulisha kwa jina la Dk. 
Rugemaleza Nshara na kupinga tuhuma zinazomkabili mteja wake kwa kudai 
ameonewa katika shauri hilo.
Kutokana na maelezo ya wakili wa upande wa utetezi, Mwenyekiti wa 
Baraza, Jaji Mstaafu Hamis Msumi, alimtaka mwanasheria huyo kuelewa kuwa
 baraza hilo si mahakama ya kisheria, na kwamba taratibu zake 
hazitofautiani na taratibu za kimahakama.
Baada ya maelezo hayo, Jaji Msumi aliutaka upande wa walalamikaji ambao 
ni Sekretarieti ya Maadili ya Viongozi wa Umma kutoa ushahidi wao, 
ambapo aliyekuwa wa kwanza kutoa maelezo yake ni Katibu Msaidizi Idara 
ya Uongozi wa Siasa wa sekretarieti hiyo, Waziri Kipache (45) aliyedai 
kuwa anamfahamu mlalamikiwa kuwa alikuwa Waziri wa Ardhi, Nyumba na 
Maendeleo ya Makazi na ni Mbunge wa Muleba Kusini.
Alisema baada ya kupata taarifa mbalimbali za kuwapo kwa baadhi ya 
viongozi wa umma kutuhumiwa kupokea fedha kutoka Kampuni ya VIP kinyume 
na maadili, alikutana na Tibaijuka na kumhoji kuhusu suala hilo.
“Baada ya taarifa hizo, tulifanya uchunguzi ili tuweze kujiridhisha kama
 kanuni na taratibu za masharti ya uongozi wa umma yamezingatiwa katika 
upokeaji wa fedha hizo.
“Tulibaini kuwa Aprili 4, mwaka 2012, Profesa Tibaijuka aliomba fedha 
kwa mke wa mmiliki wa Kampuni ya VIP, James Rugemalila na maombi hayo 
yaliwasilishwa kwa barua,” alisema Kipeche.
Shahidi huyo ambaye alitoa maelezo yake mbele ya jopo la viongozi wa 
Baraza la Maadili akitimia dakika kumi, pia alitoa barua ya Profesa 
Tibaijuka ya kuomba fedha hizo.
Alidai kuwa Profesa Tibaijuka akiwa mmoja wa wadhamini wa Bodi ya 
Wakurugenzi wa Taasisi ya Barbro Johannson Girls Trust, pia ndiye 
mmiliki wa Shule ya Kajumulo Alexandre iliyopo mkoani Kagera akiwa ni 
meneja wa shule hiyo.
“Kwa mujibu wa sheria ya maadili ya viongozi wa umma, hawaruhusiwi 
kuomba fedha kwa masilahi ya kiuchumi, hivyo basi Profesa Tibaijuka 
ametenda kosa hilo,” alisema Kipache.
Kutokana na maelezo hayo ya shahidi huyo, Jaji Msumi, aliutaka upande wa
 utetezi kuwasilisha ushahidi mbele ya baraza kuhusu madai yake hayo.
Kwa kuwa ilikuwa imetimu saa 11: 45, Jaji Msumi aliahirisha shauri hilo 
hadi mchana kwa kuwa tayari ulikuwa umefika muda wa mapumziko, huku 
akimtaka Profesa Tibaijuka na timu yake wajipange kwa maelezo na 
kuwasilisha vielelezo kutokana na tuhuma alizokuwa akituhumiwa.
Ilipotimu saa 6:30 mchana, shauri hilo liliendelea kwa Jaji Msumi 
kumsimamisha Profesa Tibaijuka atoe ushahidi wake mwenyewe na aeleze 
namna miamala ya fedha ilivyofanyika.
 
UTETEZI WA TIBAIJUKA
Akizungumza baada ya madai hayo kutolewa, Profesa Tibaijuka alipinga 
ushahidi wa Kipeche na kudai kuwa uhusiano wake na taasisi hiyo ni kuwa 
yeye ni miongoni mwa waanzilishi akiwa na mumewe.
Alisema uamuzi wa kuanzisha shule hiyo, ulitokana na kuona umuhimu wa 
kupigania elimu ya mtoto wa kike ili aweze kupata fursa ya kuendelezwa 
kielimu, kiuchumi na kijamii.
Alisema kabla ya hapo alifanya utafiti mwaka 1994 na 1995 ambapo ripoti 
yake inaonyesha kuwa mtoto wa kike hana thamani kwenye jamii, ndiyo 
maana anashindwa kupatiwa haki ya kupata elimu katika ngazi mbalimbali.
Profesa Tibaijuka alisema kutokana na utafiti huo, ndipo akafikia uamuzi
 wa kuanzisha taasisi hiyo ili aweze kuwasaidia watoto hao, hasa wale 
wenye vipaji na wanaotoka katika mazingira magumu.
“Nikiwa mkereketwa wa Umoja wa Mataifa (UN), sielewi masilahi gani 
nimepata kupitia fedha hizi, ikiwa shughuli za ‘fund rising’ sijaanza 
leo, nimeisomea kabisa nchini Marekani kwa fedha za Serikali mwaka 1980.
“Hata nilipokuwa UN nilikuwa nikifanya hivyo na aliyekuwa Katibu Mkuu wa
 Umoja wa Mataifa wakati huo, Kofii Annan, aliniruhsu na kunipongeza 
kuwa ninachokifanya ni muhimu kwa jamii,” alisema Profesa Tibaijuka.
Kutokana na maelezo hayo, aliomba apewe mwongozo nini maana ya kukiuka 
maadili ya utumishi wa umma, huku akidai kuwa amedhalilishwa, 
amefedheheshwa na kwamba anaonekana ni tapeli katika jamii, jambo ambalo
 limemsababishia kukosa amani katika nafsi yake.
“Nimeshangaa kuitwa kwenye baraza hili na kuambiwa kuwa nimekiuka 
maadili ya utumishi wa umma, kwani maadili maana yake nini? Kufanya 
shughuli za kuisadia jamii ni kukiuka maadili?
“Ninaomba mwenyekiti unisaidie katika hili ili haki itendeke dhidi 
yangu, maana nimeanza kuhukumiwa tangu niko bungeni bila hata ya kupewa 
nafasi ya kusikilizwa, nilijaribu kumwomba Mheshimiwa Spika Anne Makinda
 ili aweze kunisikiliza, lakini alikataa,” alisema.
Alisema kutokana na hali hiyo, alilishukuru baraza hilo kumwita na 
kumsikiliza kwa sababu hajawahi kupata haki yoyote ya kusikilizwa, ndiyo
 maana alikubali kwenda mwenyewe ili aweze kusema yanayomsibu.
Baada ya maelezo hayo ya Profesa Tibaijuka, walisimama wanasheria watatu
 wakiongozwa na Getrude Cyriacus, ambaye alikuwa wa kwanza kumuhoji 
kuhusu malalamiko dhidi yake kuwa aliomba fedha kwa Rugemalila na 
kuzipokea kupitia Kampuni ya VIP hali ya kuwa maadili hayaruhusu.
Swali hilo lilionekana kuwa mwiba kwa Profesa Tibaijuka, ambaye muda 
wote alikuwa akisikiliza kwa makini, ambapo alikiri kuomba fedha hizo, 
lakini si kwa masilahi yake binafsi, bali ni kwa ajili ya Taasisi ya 
Barbro Johannson Girls Trust.
Wakili Getrude: Wakati unapewa fedha hizo ulikuwa na cheo gani, ni waziri na mbunge au la.
Profesa Tibaijuka: Sioni mantiki ya swali hilo.
Baada ya kujibu, alimwangalia wakili wake, Dk. Nshala ambaye alimtaka 
alijibu swali hilo, ndipo Tibaijuka alisema kipindi anapokea fedha hizo 
alikuwa Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi na Mbunge wa 
Muleba Kusini.
Mwanasheria Hassan Mayunga alimhoji Profesa Tibaijuka kwanini alifanya 
haraka kutoa fedha hizo zilizoingizwa kwenye akaunti yake katiba Benki 
ya Mkombozi na kuzitumia katika kazi zake binafsi.
Alisema fedha hizo ziliingizwa tarehe 12 mwaka 2014 na kuanza kufanya 
miamala binafsi tarehe 14 ambapo Sh milioni mbili alizitumia kununua 
hisa Makongo Parish.
Profesa Tibaijuka alisema baada ya hapo alitoa Sh 400,000 na kununua 
hisa Kijiwe Parish na siku hiyohiyo alitoa Sh milioni 10 ambazo hazina 
maelezo sahihi.
“Sh milioni 10 nilitoa kwa ajili ya kununua mboga kwa sababu fedha hizo ni zangu.
“Nashangaa kuambiwa nimevunja maadili, kwanza fedha hizi ni ndogo japo ni hela, lakini mimi sina shida na fedha hizi.
“Mimi ni mstaafu wa miaka mingi, nina pensheni ya kila mwezi, sina shida
 na fedha hizo ndiyo maana hata hizo fedha zilizobaki kwenye akaunti 
hiyo sijaenda kuziangalia kwa sababu sina shida za hivyo,” alisema.
Kabla ya Tibaijuka kuanza kutoa maelezo yake mbele ya baraza hilo, 
Wakili wa upande wa utetezi, Dk. Rugemaleza Nshala, alisimama na 
kumuhoji shahidi Kipache na kuzua mabishano.
Dk. Nshala: Kwenye sheria ya maadili wapi inaonyesha kiongozi wa umma kupewa zawadi ni dhambi?
Kipache: Si dhambi ila kisheria inatakiwa isizidi Sh 50,000.
Dk. Nshala: Je, fedha alizopewa Tibaijuka ni zake au za taasisi?
Kipache: Ni za taasisi, lakini tatizo lililopo ni kwamba ameingiziwa 
fedha katika akaunti yake binafsi na si akaunti ya taasisi na hapo ndiyo
 amekiuka maadili.
Dk. Nshala: Je, kiongozi wa umma kuomba michango ya maendeleo kwa wadau 
ni dhambi? Mbona Waziri Mkuu Pinda alikuwa mgeni rasmi kusaidia 
kukusanya michango ya Taasisi ya Maajar Trust Fund. Je, alikiuka sheria 
ya maadili?
Kipache: Waziri Mkuu alihamasisha kutoa michango, lakini fedha 
zilizotolewa hazijaingia katika akaunti yake binafsi, tukio hilo ni 
tofauti kwa sababu fedha za Tibaijuka aliingiza kwenye akaunti yake 
binafsi.
Dk. Nshala: Kwanini hawajaenda kwenye bodi ya wadhamini kuuliza kama 
fedha hizo zimetumikaje au kwenda mbali zaidi kwenye benki ya Mkombozi 
kuulizia miamala?
Kipache: Hatukuona umuhimu wa kwenda kwa sababu waliokuwa na ‘statement’
 ya benki ilionyesha miamala yote iliyofanyika kwa Tibaijuka, lakini pia
 tulikwenda Rita kufanya uchunguzi ili kuweza kuangalia usajili wa 
taasisi hii na wamiliki wake.
SHAHIDI WA TIBAIJUKA
Naye shahidi wa Profesa Tibaijuka ambaye ni Mjumbe wa Bodi ya Wadhamini 
wa Taasisi ya Barbro Johannson Girls Trust, Balozi Paul Rupia, alisema 
fedha hizo zimetafutwa na Profesa Tibaijuka na kutoa taarifa kwenye bodi
 hiyo kuwa kuna fedha zimeingia ambazo zinatakiwa kulipwa madeni.
Alisema bodi hiyo haijampa masharti yoyote ya kumaliza kulipa madeni 
hayo na kwamba hawakuwa na sababu ya kumfuatilia kwa sababu walimwamini 
kutokana na juhudi zake binafsi za kupata fedha hizo.
Katika shauri hilo lililoanza saa 3:00 asubuhi na kuendelea hadi saa 
11:45 jioni, Profesa Tibaijuka alitoa ushahidi kwa zaidi ya saa tatu 
kuanzia saa 6:30 mchana hadi saa 9:30 alasiri.
Shauri hilo limehairishwa hadi Machi 13, mwaka huu baada ya wakili wa 
Profesa Tibaijuka kuomba hudhuru ya kwenda nchini Marekani kwa siku 
kumi.
Jaji Msumi alikubali ombi hilo na kudai kuwa shauri hilo litaendelea 
siku hiyo na kutolewa hukumu huku baraza hilo likiamua namna ya kujadili
 shauri hilo, kwamba itaamuliwa kama liwe la uamuzi wa ndani au 
hadharani.
Idadi kubwa ya watu walijitokeza katika Ukumbi wa Karimjee kusikiliza shauri hilo.
- Blogger Comment
 
- Facebook Comment
 
Subscribe to:
Post Comments
                            (
                            Atom
                            )
                          

0 comments:
Post a Comment