Dk. Slaa awasilisha maboksi 17


YANAHUSU MAONI YA KATIBA, WARIOBA AGOMA
TUME ya kukusanya maoni ya Katiba mpya inayoongozwa na Jaji mstaafu, Joseph Warioba, jana imegoma kupokea maboksi 17 ya maoni yaliyokusanywa na Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA) na badala yake ikapokea vitabu viwili vya randama kwa ajili ya maoni hayo.
Kutokana na tume hiyo kukataa kupokea ushahidi wa kile kilichoandikwa katika randama mbili zilizowasilishwa na CHADEMA, chama hicho kupitia kwa Katibu Mkuu wake, Dk. Willibrod Slaa, kimesema mpango huo unaashiria dhamira ya tume hiyo kuvibeba vyama ambavyo havina ushahidi wa ukusanyaji wa maoni kutoka kwa wananchi.
Maoni hayo ya wananchi kuhusu rasimu ya Katiba, yamekusanywa kupitia mikutano mbali mbali iliyofanywa na CHADEMA yalifikishwa katika ofisi za tume jana majira ya saa 5:56 asubuhi yakiwa katika gari aina ya Range Rover yenye namba T 162 CDA, ambapo ndani ya gari hilo alikuwamo Dk. Slaa, huku maofisa wengine wa CHADEMA wakiwa katika magari tofauti.
Mara baada ya kukabidhi maoni hayo ya wananchi, Dk. Slaa alisema amesikitishwa na hatua ya tume hiyo kushindwa kubaki na maoni yaliyokusanywa kupitia taasisi zinazoeleweka kwa kile alichoeleza kuwa kuna uwezekano mkubwa wa tume hiyo kupokea maoni ya watu waliojifungia ndani na kusema maoni hayo yametoka kwa wananchi.
Alisema tume inaweza kuibua maswali kutoka kwa taasisi na wananchi namna inavyoweza kujiridhisha na maoni yanayofikishwa kwao kwa kile alichoeleza kushindwa kupokea maoni ya awali kutoka kwa wananchi.
Aidha, Dk. Slaa alisikitishwa na utaratibu wa tume hiyo kushindwa kuwa na mpango maalumu wa kupokea maoni na kuweka kumbukumbu ya upokeaji huo.
“Sijui kama hawa watu walijipanga juu ya upokeaji wa maoni, angalia sisi kama tusingelazimisha watugongee muhuri kwa ajili ya uthibitisho wa upokeaji tungeondoka hivi hivi, sasa hali hii wamefanyiwa watu wangapi ambao hawana kitabu cha kusaini?” alihoji Dk. Slaa.
Aliongeza kuwa katika randama walizowasilisha kwa tume, wameweka hoja 66 baada ya kujiridhisha na hoja nyingine zilizoko katika rasimu ya Katiba yenye hoja 240.
Alisema hoja ambazo hazijaguswa katika randama waliyowasilisha ni zile ambazo zinakubaliwa na CHADEMA pamoja na wananchi waliotoa maoni kupitia mikutano ya CHADEMA.
Namna walivyopata maoni
Kuhusu idadi ya watu waliotoa maoni yaliyowasilishwa jana, Dk. Slaa alisema hadi juzi walipokuwa wakifunga randama, kulikuwa na watu zaidi ya milioni 3.4 waliotoa maoni kwa njia mbalimbali.
Alitaja njia hizo kuwa ni mabaraza ya wazi ambapo walikusanya maoni ya watu 3,200,889 kutoka katika majimbo 81 waliyoyafikia, katika mabaraza ya ndani walifika kata 586 na kukusanya maoni 11,7274.
Njia nyingine zilizotajwa na Dk. Slaa ni ngazi ya majimbo ambapo walifanya mikutano ya ndani katika majimbo 189 ya Tanzania Bara na kukusanya maoni 130,000, kwa njia ya barua pepe walipata watu 612 waliotoa maoni huku kukiwa na ujumbe mfupi wa simu kutoka kwa watu 12,345 pamoja na mitandao ya kijamii na kufanya jumla ya watu waliotoa maoni kuwa 3,462,805.
Dk. Slaa alisema ushahidi wa maoni hayo upo wazi kwao na kuwataka tume ijiridhishe kwa vyama vingine vinavyosema wameshakusanya maoni ya watu zaidi ya milioni mbili.
“Sisi tumefanya haya na wenzetu walete ushahidi kama huu badala ya kukaa vyumbani na kuwatengenezea Watanzania maoni na vitu vya kuingizwa katika Katiba. Hapa tunaililia Tanzania tuitakayo na si kwa masilahi ya chama chochote,” alisema Dk. Slaa.
Aliongeza kuwa mazingira na matamko yanayotolewa na Chama Cha Mapinduzi kuwa wamekusanya maoni ya wananchi wengi na hayawezi kufikiwa na vyama vingine yana nia mbaya kwa nchi na hayaleti taswira nzuri kwa tume.
Usiri wa Tume kwa waandishi
Dk. Slaa pia alisema licha ya tume kuweka suala la uwazi kuwa ni moja ya tunu za taifa, bado imeshindwa kudhihirisha uwazi huo kwa kuwazuia waandishi wa habari kuingia na kushuhudia makabidhiano yanayofanywa katika ofisi za tume.
Alisema suala la Katiba ni la Watanzania wote na vyombo vya habari ni mhimili mkubwa wa serikali usio rasmi wenye kutegemewa kwa kiasi kikubwa na wananchi kutoa taarifa sahihi, lakini vinapozuiwa kushuhudia matukio hayo kwa uwazi ni kuwanyima fursa Watanzania kupata habari sahihi.
Aliongeza kuwa kama tume ya Katiba inafanya usiri katika kupokea maoni ya wananchi, wanaweza vipi kuwaridhisha Watanzania kuwa maoni waliyotoa ndiyo yaliyofanyiwa kazi.
Kuhusu Kingunge
Akizungumzia kauli ya Kingunge Ngombale- Mwiru, aliyoitoa juzi kuhusu umuhimu wa serikali mbili, Dk. Slaa alisema Watanzania wanapaswa kumsamehe mzee Kingunge kwa kuwa sasa amechoka.
Alisema katika vitu alivyopaswa kuvifanya Kingunge katika muda wake wa utumishi serikalini ni pamoja na kusimamia kero mbali mbali zinazolalamikiwa leo, hivyo kuendelea kuwaambia wananchi wasifikirie juu ya muundo wa Muuungano ni kuwakosea heshima.
“Mimi ninamsamehe mzee wangu huyu ila atambue muungano ulio bora ni ule unaoridhiwa kwa hiari na si kulazimisha mfumo unaoonekana una matatizo,” alisema Dk. Slaa.
  @Chadema Blog
Share on Google Plus

About Unknown

This is a short description in the author block about the author. You edit it by entering text in the "Biographical Info" field in the user admin panel.
    Blogger Comment
    Facebook Comment

0 comments:

Post a Comment