Kingunge amgeuka Kikwete: ASHAMBULIA WAZEE WANAOSHABIKIA MFUMO WA SERIKALI TATU


MWANASIASA mkongwe aliyewahi kuwa swahiba na mshauri mkuu wa Rais Jakaya Kikwete, Kingunge Ngombale Mwiru, ametoa kauli nzito inayoonyesha hakubaliani na msimamo wa Rais Kikwete na Chama cha Mapinduzi (CCM).
 
Akizungumza na waandishi wa habari jijini Dar es Salaam jana, Kingunge akimkejeli Rais na chama chake, ambacho yeye ni mmoja wa waasisi, alisema walikurupuka kukubali na kuanzisha mchakato wa Katiba mpya.
 
Kwa mujibu wa Kingunge, kabla ya Rais Jakaya Kikwete kutangaza na kuanzisha mchakato wa Katiba mpya, CCM haijawahi kufanya kikao na kuamua kuhusu suala hilo, kama walivyofanya kabla ya mchakato wa kuingia kwenye mfumo wa vyama vingi mwaka 1991.
Mbali na kumshangaa Kikwete na chama chake, vile vile Kingunge aliwashambulia wazee wenzake wanaounga mkono mapendekezo ya rasimu ya Katiba mpya kuhusu muungano wa serikali tatu.
 
Katika hali isiyo ya kawaida, Kingunge alisema wazee hao ni “sawa na watu waliochanganyikiwa”.
Anasema msimamo wake unatokana na ukweli kuwa CCM haijawahi kuwa na ajenda ya kuandika Katiba mpya na kwamba ndiyo maana suala hilo halikuwa kwenye ilani ya uchaguzi ya CCM 2010.
Alisema hoja ya Katiba mpya ni ya wapinzani, hasa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA).
Kingunge alisema kimsingi aliyeafikiana na hoja ya wapinzani kuhusu Katiba mpya ni Rais, si CCM.
Kuhusu wazee hao ambao alisema “wamechanganyikiwa” Kingunge alisema anashangaa kuona wazee ni miongoni mwa wanaopendekeza muundo wa serikali tatu, kwani baadhi yao walishiriki katika kuunda mfumo huu uliopo ambao umedumu tangu mwaka 1964.
Alisema muungano wa serikali mbili umeleta mafanikio kwa kujenga udugu na umoja wa kitaifa na kwamba kwa sababu hiyo ungeachwa uendelee badala ya kupiga kelele kwamba ufutwe, ziletwe serikali tatu.
 
Alisema baadhi ya viongozi wameshindwa kuthamini mafanikio ya muungano na sasa mawazo yao yote yamekuwa yakielekezwa kwenye vyeo vyenye marupurupu.
Aidha alipinga kauli za baadhi ya viongozi wanaosema kuwa kuwepo kwa serikali tatu kutasaidia kuimarisha muungano. Alisema serikali tatu zitaua muungano.
Kingunge aliongeza kuwa kama serikali mbili ni sababu za kufa muungano huo, basi usingeweza kudumu kwa miaka 50 sasa.
 
“Huu ni mpango wa wakubwa kutaka kujiwekea mazingira ya vyeo, kwani wapo ambao tayari wamekwishajiandaa kuwania urais wa Tanganyika.
“Nilishangaa sana hata huko bungeni watu wanapeana sifa za kuwa fulani anastahili kuwa Rais. Huu ni upotoshaji mkubwa kwa taifa,” alisema, akirejea kauli iliyotolewa juzi na Waziri asiyekuwa na wizara maalumu, Profesa Mark Mwandosya, aliyemfagilia Spika wa Bunge, Anna Makinda, kwamba anafaa kuwa Rais.
 
Kingunge aliongeza kuwa kwa maoni yake lazima Katiba mpya iweke mipango ya maendeleo ambayo itashirikisha wananchi wa ngazi zote.
Kingunge alisema isiwe mipango hiyo inapangwa na viongozi kutoka juu na kuishusha chini bila kujua wanahitaji nini kabla.
Alisema Katiba inayotakiwa ni ile itakayosimamia na kupatikana kwa maendeleo yanayofanana kati katika jamii.
Kuhusu uraia wa nchi mbili, Kingunge alisema suala hilo lilikuwa linasemwa pembeni lakini sasa wanataka suala liingizwe kwenye Katiba.
“Mwanzo nilijua ni utani lakini nilishangaa suala hili kubwa kuliona limeingizwa kwenye kijitabu kilichotolewa na chama changu na kupendekeza hivyo,” alisema.
Alisema suala la uraia ni la nchi, hivyo chama kilipaswa kutoa nafasi kwa wananchi kujadili kwa kina jambo hilo na sio viongozi kujiamulia wenyewe.
“Kwa mfano nchi yetu ilipovamiwa na Nduli Idd Amini kama kungekuwa na vijana wenye uraia wa nchi mbili wangejiweka upande gani, hii ni mipango ya watu wanaopenda kunogewa na maisha kwenye nchi za watu,” alisema.
Alisema amekuwa kwenye Halmashauri Kuu ya Taifa (NEC) ya CCM kwa muda mrefu lakini hakuwahi kusikia hata siku moja kujadiliwa suala hilo ambalo ameliita kuwa la hatari.


CHADEMA
Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA), kimeeleza kuiunga mkono rasimu hiyo kwa asilimia 80 kulingana na maoni ya watu milioni 3.4 waliokusanya.
Hata hivyo, CHADEMA imeainisha hoja 11 ambazo wananchi wamependekeza ziongezwe katika rasimu hiyo ya Katiba mpya.
Akizungumza na waaandishi wa habari jana makao makuu ya chama hicho, Katibu Mkuu wa CHADEMA, Dk. Willibrod Slaa alisema mrejesho huo umepatikana baada ya kuwazungukia wanachama wao na Watanzania wengine kwa wiki mbili.
Dk. Slaa alisema maoni hayo yamekusanywa kupitia kanda 10 za chama hicho na Watanzania waishio nje ya nchi kwa njia ya kisayansi huku yakiwa na vithibitisho tofauti na vyama vingine vya kisiasa.
 
Huku akieleza kuwa bado wanakusanya takwimu za Watanzania walioandika ambazo zinatoka mkoani, hadi jana walikuwa wamekusanya maoni kutoka katika mabaraza ya Katiba 117,274 yaliyoendeshwa na madiwani.
Alisema kuwa waliendesha mabaraza ya wazi 3,200,889, ya ndani 130,004 na kukusanya maoni yaliyotumwa kwa njia ya barua pepe 612, ujumbe kwa njia ya simu za mikononi 12,345 na mitandao ya kijamii 1,681.
Dk. Slaa alisema katika ziara hiyo, watanzania walisisitiza mambo 11 ambayo yapo katika rasimu hiyo na mapya kwa ajili ya kuongezwa kwa lengo la kuboresha rasimu hiyo kuwa ni pamoja serikali tatu yaani ya Jamhuri ya Muungano, Tanganyika na Zanzibar.
Pili, ni kuitaja na kuiweka katika Katiba mpya mipaka ya Tanganyika na Zanzibar ili kudumisha amani ya nchi hizo na jirani zao.
 
Kuhakikisha haki ya kila raia wa Jamhuri ya Muungano aliyetimiza umri wa miaka 18 kupiga na kupigiwa kura katika uchaguzi wowote unaofanywa katika jamhuri.
Hoja zingine ni swala la haki ya kupatiwa malipo ya uzeeni pamoja na msaada wa hifadhi ya jamii kwa gharama ya serikali wakati wa uzeeni, haki ya kupatiwa msaada wa matibabu, haki ya jamii kumiliki rasilimali za asili kama vile ardhi, madini, mafuta na gesi asilia, maji na misitu na wanyamapori vitumike kwa manufaa ya Watanzania.
“Iwe marufuku kwa mamlaka ya serikali ya jamhuri za washirika wake kutwaa rasilimali asili kwa malengo ya kuzigawa kwa wawekezaji au kwa malengo yoyote bila ya kupata ridhaa huru na ufahamu wa wananchi wanaoishi kwenye eneo zinakopatikana rasilimali hizo,” alisema.
 
Pia suala la uraia wa nchi mbili, mtu hatapoteza uraia wa Jamhuri ya Muungano kwa sababu tu ya kuwa na uraia wa nchi nyingine.
Yapo pia masuala ya muungano yaani maadili na miiko ya uongozi na utumishi wa umma, haki za binadamu na wajibu wa raia, tume huru ya taifa ya uchaguzi na masuala yote yanayohusu uchaguzi.
 
“Tume huru ya uchaguzi itatangaza matokeo ya uchaguzi wa Rais haraka iwezekanavyo na kwa vyovyote vile kabla ya kupita siku saba tangu tarehe ya uchaguzi huo.
“Rais mteule atakabidhiwa madaraka ndani ya siku tisini baada ya kutangazwa kuwa ameshinda, wakati wote Rais akiwa madarakani na baada ya kuacha kushika madaraka hayo anaweza kushtakiwa kwa ajili ya kosa lolote la jinai chini ya sheria au chini ya mkataba wowote wa kimataifa ambao jamhuri ya muungano ni mwanachama,” alisema.
Alitaja hoja ya kumi kuwa ni siku ya kupiga kura isiwe ni siku ya kuabudu ya imani ya dini yoyote ile, bali iwe siku ya kazi ambayo itapaswa kutangazwa kama siku ya mapumziko.
Dk. Slaa alisema pamoja na ibara 68 za rasimu ambazo zimetolewa na Tume ya Mabadiliko ya Katiba, CHADEMA wakati inazunguka imekutana na mambo 11 hayo ambayo yalikuwa yakisisitizwa na wananchi.
 
NCCR-Mageuzi
Chama cha NCCR-Mageuzi kimependekeza kuwepo na serikali tatu ya Tanganyika, Zanzibar na Shirikisho itakayokuwa chini ya mkataba wa kimataifa.
Pia alisifu usikivu wa Tume ya Mabadiliko ya Katiba chini ya Jaji Joseph Warioba kutokana na kurasimu baadhi ya mapendekezo ya chama hicho katika ushiriki wake kuhusu utayarishaji wa rasimu hiyo.
Akizungumza na waandishi wa habari jana jijini Dar es Salaam, Kaimu Katibu Mkuu wa chama hicho, Mosena Nyambabe, kuhusu maoni na mapendekezo yao kwa tume, alisema wameona kuna haja ya kurejeshwa kwa nchi ya Tanganyika itakayokuwa na mamlaka yake kamili sawa na Zanzibar.
Alisema chama hicho kimeona umuhimu wa mapendekezo 18 ya Muungano yaliyoakisiwa na Tume ya Mabadiliko kupewa kipaumbele zaidi.
Aliyataja mambo hayo kuwa ni pamoja na suala la Katiba na mamlaka ya Jamhuri ya Muungano, Ulinzi na Usalama, sarafu za Benki kuu, mambo ya nje, vyama vya siasa, ushuru wa bidhaa na mapato ya kodi yatokanayo na mambo ya muungano.
HABARI kwa  Hisani ya Chadema Blog.
Share on Google Plus

About Unknown

This is a short description in the author block about the author. You edit it by entering text in the "Biographical Info" field in the user admin panel.
    Blogger Comment
    Facebook Comment

0 comments:

Post a Comment