MFUMUKO WA BEI NCHINI WAPANDA ZAIDI YA MWEZI ULIOPITA!!


Mkurugenzi wa Takwimu za Jamii na sensa ya Watu na Makazi Bw. Ephraimu Kwesigabo akizungumza na waandishi wa habari leo jijini Dar es salaam kutoa taarifa ya mfumuko wa bei nchini unapimwa kwa kipimo cha mwezi.

( Na. Aron Msigwa/MAELEZO - Dar es salaam)
Ofisi ya Taifa ya Takwimu imeeleza kuwa mfumuko wa bei nchini  kwa mwezi Machi umeongezeka ikilinganishwa na mwezi uliopita kutokana na kupanda kwa bei za bidhaa na huduma mbalimbali. 

 Akizungumza na waandishi wa habari leo jijini Dar es salaam Mkurugenzi wa Takwimu za Jamii na sensa ya Watu na Makazi Bw. Ephraimu Kwesigabo amesema kuwa mfumuko wa bei wa Taifa kwa mwezi Machi 2014 umeongezeka na kufikia asilimia 6.1 kutoka asilimia 6.0 mwezi uliopita.

Amesema  kuwa kasi ya upandaji wa bei za bidhaa na huduma kwa mwezi Machi 2014 imeongezeka kidogo ikilinganishwa na ile iliyokuwepo mwezi Februari  huku kukiwa na ongezeko dogo la upandaji wa bei  kwenye baadhi ya bidhaa na huduma mwezi huu ikilinganishwa na bei za mwezi Machi mwaka jana.

 Ameeleza kuwa mfumuko wa bei za bidhaa za vyakula na migahawa kwa mwezi Machi umeongezeka hadi asilimia 7.9 kutoka asilimia 6.9 za mwezi Februari mwaka huu huku badiliko la fahirisi za bidhaa zisizo za vyakula likipungua hadi asilimia 5.2 kwa mwezi Machi 2014 kutoka asilimia 6.2 za mwezi Februari.

Amefafanua kuwa mwenendo wa bei za bidhaa za vyakula kama samaki, mbogamboga, ulezi na matunda, ndizi za kupika na maharage zimeonyesha kuongezeka kwa kiwango kikubwa kwa mwezi Machi ikilinganishwa na bei za bidhaa hizo kwa mwaka uliopita huku bei za bidhaa zisizo za vyakula za vitambaa vya suti za wanaume, gharama ya usafi wa nywele na usafi binafsi, Petroli, mkaa, huduma za matibabu pamoja na tiketi za kutazama mpira wa miguu ligi kuu  zikionyesha ongezeko.

Kwa upande wa  mfumuko wa bei unaopimwa kwa kipimo cha mwezi,ameeleza kuwa kumekuwa na ongezeko dogo kwa asilimia 0.6 ikilinganishwa na ongezeko la asilimia 1.4  kwa mwezi Februari mwaka huu, huku fahirisi za bei za taifa zikiongezeka hadi kufikia 149.49 kwa mwezi Machi kutoka 140.93 za mwezi Machi mwaka uliopita huku fahirisi za zinazopimwa kwa kipimo cha mwezi zikifikia asilimia 149.49 kutoka 148.62 za mwezi uliopita.

Amezitaja bidhaa zilizochangia ongezeko la fahirisi za bei nchini  kuwa ni pamoja na nyanya, viazi vitamu, matunda, mchele, tambi na kuku wa kisasa ambao wameongezeka kwa asilimia 1.8.

 Aidha kufuatia hali hiyo  ya mfumuko wa bei Bw. Kwesigabo ameeleza kuwa  uwezo wa shilingi 100 ya Tanzania katika kununua bidhaa na huduma za jamii kwa mwezi Machi umepungua na kufikia shilingi 66 na senti 90.

“Kupungua kwa thamani ya Shilingi kunamaanisha kwamba, kama mtu alikuwa na uwezo wa kununua bidhaa kwa Shilingi 100 mwaka jana, basi kwa mwaka huu itampasa aongeze zaidi ili aweze kununua kitu kama kile kile, kwa mfano badala ya shilingi 100 inabidi atumie shilingi 134”

Kuhusu ulinganifu  mfumuko wa bei wa Tanzania na baadhi ya nchi za Afrika Mashariki amesema kuwa una mwelekeo unaofanana na kueleza kuwa mfumuko wa bei nchini Kenya umepungua kidogo na kufikia asilimia 6.27 kwa mwezi Machi  kutoka asilimia 6.86 za mwezi Februari,  huku  Uganda ikiwa na mfumuko wa asilimia 7.1 kwa mwezi Machi ikilinganishwa na asilimia 6.8 za mwezi uliopita.
Share on Google Plus

About Unknown

This is a short description in the author block about the author. You edit it by entering text in the "Biographical Info" field in the user admin panel.
    Blogger Comment
    Facebook Comment

0 comments:

Post a Comment