MNYIKA ASIKITISHWA NA MAJIBU YA MKUU WA MKOA WA DAR KUHUSU BODABODA NA BAJAJI


MBUNGE wa Ubungo, John Mnyika (CHADEMA), ameeleza kutoridhishwa na majibu yaliyotolewa na Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, Said Meck Sadiq, kuhusu mgogoro unaoendelea juu ya usafiri wa pikipiki ‘bodaboda’ na bajaj

.Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, amenukuliwa na vyombo vya habari akisema hawezi kusitisha kwa muda agizo lake la kukataza vyombo hivyo vya usafiri kuingia katikati ya jiji kwa kuwa si agizo lake bali ni sheria.
 
Mnyika alisema jana kuwa mkuu huyo wa mkoa alitoa kauli hiyo kutokana na kumuandikia ujumbe, akimtaka asitishe kwa muda utekelezaji wa tamko lake, ili kupisha mazungumzo kati ya serikali, wahusika wa bodaboda, bajaj na wadau wengine.
“Nimepitia sheria inayohusika ambayo ni The Surface and Marine Transport Regulatory Authority Act, Sheria namba 9 ya mwaka 2001, hakuna kifungu chochote kinachokataza pikipiki au bodaboda na bajaj kuingia katika maeneo ya katikati ya jiji, hivyo mkuu wa mkoa anapaswa kutoa ufafanuzi kwa umma ni sheria ipi anaitumia,” alisema Mnyika katika taarifa yake kwa vyombo vya habari jana.
Alisema Sadiq anapaswa kuzingatia kwamba sheria hiyo kifungu cha 5 imetamka kwamba wajibu wa Mamlaka ya Udhibiti wa Usafiri wa Nchi Kavu na Majini (Sumatra) ni kulinda maslahi ya watumiaji wa huduma na kuhamasisha upatikanaji wa huduma, ikiwemo kwa wateja wa kipato cha chini.
“Usafiri wa pikipiki/bodaboda na bajaj sio tu umetoa fursa ya ajira kwa vijana, bali pia unasaidia wananchi wa kipato cha chini na pia unasaidia katika mazingira ya foleni katika Jiji la Dar es Salaam, hivyo agizo la kutaka usafiri huo uishie Buguruni, Ubungo, Tazara na Chuo cha Uhasibu ni suala ambalo limeibua mgogoro unaostahili ufumbuzi wa haraka,” alisema Mnyika.
 
Alieleza Mnyika kuwa anatambua kwamba vifungu vya 6, 38 na 39 vya sheria hiyo vimetoa fursa ya mamlaka zinazohusika kutunga kanuni mbalimbali na kwamba ielewe kanuni hizo sio sheria, hivyo kauli ya mkuu wa mkoa haiwezi kusitisha sheria.
 
Aliongeza hali hiyo inaleta hisia miongoni mwa watumiaji, waendeshaji na wamiliki wa pikipiki/bodaboda na bajaj, kwamba pengine zipo sababu nyingine za ziada ambazo mkuu wa mkoa anapaswa kuzieleza wazi badala ya kusingizia sheria.
Alisema anakusudia kumwandikia barua rasmi kutaka kuitishwe kikao cha Baraza la Ushauri la Mkoa (RCC) ambalo litakutanisha pamoja Sekretariati ya Mkoa, Halmashauri ya Jiji, Halmashauri za Manispaa zote za Jiji la Dar es Salaam, Sumatra na mamlaka nyingine zinazohusika, ili kupatia ufumbuzi mgogoro huo.
 
Pia aliongeza ili fedha za umma ziweze kutumika vizuri, katika barua yake ya kupendekeza ajenda, atapanua wigo wa mjadala wa matatizo ya usafiri katika Jiji la Dar es Salaam ili masuala yote ya kisheria yaweze kujadiliwa na maazimio ya utekelezaji kuweza kupangwa.
Mbunge huyo ameongeza kuwa tayari ameshawaandikia ujumbe wabunge wenzake wa Dar es Salaam, waweze kuunga mkono ajenda hiyo kujadiliwa na ufumbuzi uweze kupatikana kwa maslahi ya vijana na wasafiri katika jiji hilo.
Share on Google Plus

About Unknown

This is a short description in the author block about the author. You edit it by entering text in the "Biographical Info" field in the user admin panel.
    Blogger Comment
    Facebook Comment

0 comments:

Post a Comment