|  | 
| Mwenyekiti wa iliyokuwa Tume ya Mabadiliko ya Katiba, Jaji Joseph Warioba | 
WAZIRI Mkuu Mstaafu na 
aliyekuwa Mwenyekiti wa Tume ya Mabadiliko ya Katiba, Jaji Joseph 
Warioba, amekosoa kitendo kilichofanywa na bunge wakati wa kutoa 
mapendekezo ya waliohusika na mgawo wa fedha za Tegeta Escrow, akisema 
walikiuka katiba kwa kuingilia mamlaka ya mhimili mwingine.
Akizungumza katika 
kipindi cha dakika 45 kilichorushwa na televisheni ya ITV, juzi alisema 
Jaji Warioba kilichotokea bungeni wakati wa sakata la escrow ni matokea 
ya kupingwa kwa mambo muhimu waliyokuwa wameyaweka kwenye rasimu ya Tume
 ya Mabadiliko ya Katiba.
Alisema maoni ya 
wananchi yalitaka kuheshimiwa kwa mgawanyo wa madaraka kwa kila mihimili
 kuheshimu mwingine, hivyo bunge katika sakata hilo halikupaswa kutoa 
maazimio ya kufukuza watendaji wa serikali kama lilivyofanya.
"Bunge'' kazi yake kwa mujibu wa katiba ni kuisimamia serikali si kufukuza watendaji wa serikali, si sawa na wala si haki kwani Serikali ni mhimili kamili kikatiba unaojitegemea, unaopaswa kuheshimiwa na una mkuu wake ambaye ni Rais...ambaye hapaswi kulazimishwa kufanya jambo,"alisema.
Alisema Katiba 
iliyokuwa imependekezwa na wananchi ililenga kuondo migongano kama hiyo 
ambayo imekuwa ikikumba nchi. Alisema kitendo cha wabunge kutoa maazimio
 ya kufukuza watendaji wa Serikali wakijua kuwa wanaosema wafukuzwe nao 
ni wabunge wenzao si sawa.
Alisema suala la katiba
 mpya bado lipo mikononi mwa wananchi na serikali haipaswi kukata tamaa 
kwa lolote litakalotokea ambapo hatua iliyofikiwa itaheshimiwa na wakati
 wowote kama itashindikana mwaka huu itafanikiwa wakati mwingine.
Amesema sheria ya maadili ya viongozi wa umma 
haina nguvu ya kukabiliana na mmomonyoko huo na  inakosa meno kwa sababu
 inasimamiwa na watu walewale wasiotaka ‘kuguswa’.
“Hatuwezi kuendelea kama ilivyo sasa bila kuchukua
 hatua kali na nzito kushughulikia maadili. Lazima kuna siku suala hili 
litaingia katika Katiba tu,” alisema.
Jaji Warioba ametoa kauli hiyo ikiwa zimepita siku
 mbili tangu Baraza la Sekretarieti ya Maadili ya Viongozi wa Umma 
kutaja viongozi wa umma itakaowahoji kutokana na kuhusika katika kashfa 
ya Akaunti ya Tegeta Escrow.
Miongoni mwao yupo kigogo wa Ikulu mwenye cheo cha
 mnikulu, Shaban Gurumo, aliyekuwa Waziri wa Ardhi Nyumba na Maendeleo 
ya Makazi, Profesa Anna Tibaijuka na aliyekuwa Waziri wa Nishati na 
Madini, Profesa Sospeter Muhongo na mwanasheria mkuu wa zamani, Andrew 
Chenge.
Katika rasimu ya pili ya Katiba, Tume ya Jaji 
Warioba ilipendekeza miiko na kanuni za uongozi kama tunu za Taifa, 
lakini Bunge Maalumu la Katiba iliyaondoa na kuyaweka katika msingi wa 
utawala bora.
Mara kadhaa Jaji Warioba amekuwa akihoji kuwa 
uzalendo na uadilifu si mpaka mtu awe kiongozi, kwamba mambo hayo mawili
 si misingi ya utawala bora ni misingi ya kitaifa na inamhusu kila 
Mtanzania.
Akifafanua zaidi suala la maadili katika kipindi 
hicho, Jaji Warioba alisema tume yake iliangalia sheria ya maadili 
ikaona haina nguvu sana na inategemea kiongozi mmoja na ndiyo maana 
waliingiza suala hilo katika rasimu ya Katiba.
“Tuna sheria ya maadili lakini haina nguvu kwa 
sababu wanaoisimamia ni walewale. Nchi za Ufilipino (Philippines), 
Afrika Kusini, Namibia na Kenya walikuwa na sheria lakini haikuwa na 
nguvu na iliwahusu watu walewale. Waliamua kuweka maadili katika Katiba 
ili waweze kulitekeleza vizuri,” alisema.
Alisema maadili pia yanawahusu viongozi lakini 
wakati huo huo viongozi hao ndiyo wanaosimamia sheria ya maadili, hivyo 
hawawezi kukubali liwemo jambo litakalowadhuru.
Jaji Warioba alieleza jinsi Azimio la Arusha 
lilivyokuwa na nguvu, akifafanua kuwa suala la maadili lilijipambanua 
wazi  na waliokuwa wakitenda mambo kinyume walijiondoa wenyewe bila 
kusubiri kuondolewa.
Akigusia suala la maadili na sakata la mabilioni ya fedha yaliyochotwa katika Akaunti ya Tegeta Escrow alisema, “Katika suala la escrow niliuliza nani msafi…, we subiri tu si tunakwenda katika uchaguzi mkuu viongozi watakuwa na fedha nyingi sana.”
                
              
                
              
                
              
Akigusia suala la maadili na sakata la mabilioni ya fedha yaliyochotwa katika Akaunti ya Tegeta Escrow alisema, “Katika suala la escrow niliuliza nani msafi…, we subiri tu si tunakwenda katika uchaguzi mkuu viongozi watakuwa na fedha nyingi sana.”
Akizungumzia daftari wa wapigakura na upigaji wa 
Kura ya Maoni kupitisha Katiba Inayopendekezwa, alisema, “Nia ya 
kupitisha Katiba mpya mapema ilikuwa na lengo la kuitumia katika 
Uchaguzi Mkuu wa Oktoba, lakini inahitaji maandalizi. Mfano Katiba 
Inayopendekezwa ina sehemu ya Tume ya Uchaguzi na kama ukiipitisha, 
utaunda upya tume hiyo na suala hilo linahitaji muda.”
Alisema ili kufanikisha uundwaji wa tume hiyo ni 
lazima Bunge likutane, lakini mpaka itakapofika siku ya kuipigia kura 
Katiba hiyo na kuipitisha, Bunge litakuwa limekwishakaa na hakutakuwa na
 uwezekano wa kubadili lolote.
“Hakuna haja ya kuharakisha, ni vizuri twende taratibu ili tusije tukafanya makosa ambayo yatatuletea matatizo,” alisema.
Aliongeza, “Itakuwa vizuri kama kura ya maoni 
ikasitishwa mpaka mwaka 2016. Inaonekana tutalazimika kusubiri na hii 
inatokana na matatizo tu ya kawaida ya kutokuwa na daftari la 
Wapigakura.
Jaji Warioba pia aligusia kitendo cha wajumbe wa 
Bunge Maalumu la Katiba kuruhusiwa kugombea nafasi za kisiasa baada ya 
kumalizika kwa Bunge hilo, akisema kuwa hilo lilikuwa kosa kubwa.
“Uganda tume ilipomaliza kazi, wananchi walichagua
 Bunge la Katiba na sharti moja ni kwamba ukiingia katika Bunge hilo 
hauruhusiwi kugombea uongozi. Walijua kazi yao ni kupitisha Katiba tu,” 
alisema.
Alisema kosa lililofanyika nchini ni kuruhusu 
wabunge waliopitisha Katiba kugombea, hivyo kuwafanya baadhi kuondoa 
masuala ya msingi waliyoona kuwa ni kikwazo kwao katika uchaguzi.
“Nadhani hiyo ni kasoro tuliyokuwa nayo na tulipeleka watu ambao wana malengo na Katiba kwa manufaa yao binafsi,” alisema.
Kuhusu maridhiano kuelekea upigaji wa Kura ya 
Maoni alisema, “Suala la maridhiano lilipofika kwenye vyama vya siasa 
likabadilika na sasa tunazungumzia maridhiano ya vyama vya siasa. 
Maridhiano ya vyama vya siasa siyo lazima yawe maridhiano ya wananchi.”
Jaji Warioba pia alizungumzia suala la muungano, kueleza historia ya mfumo wa uteuzi wa viongozi wa Serikali ya Muungano na Zanzibar ili kuondoa dhana ya upande mmoja kuonekana unatoa viongozi wengi kuliko mwingine.
Jaji Warioba pia alizungumzia suala la muungano, kueleza historia ya mfumo wa uteuzi wa viongozi wa Serikali ya Muungano na Zanzibar ili kuondoa dhana ya upande mmoja kuonekana unatoa viongozi wengi kuliko mwingine.
0 comments:
Post a Comment