WABUNGE WAWAJIA JUU MAWAZIRI DODOMA!!

 
Mwenyekiti wa Kamati ya Bunge ya Ardhi, Maliasili na Utalii, James Lembeli akiwasilisha bungeni taarifa ya kamati yake katika kikao cha sita cha mkutano wa 18 wa Bunge, Dodoma.

Wabunge jana waliwaweka kitimoto mawaziri wanne wakiwataka watoe maelezo ya kukwama kwa baadhi ya mambo katika wizara zao na kusababisha matatizo kwa wananchi na Serikali kukosa fedha.
 
Mawaziri hao ni wa Maliasili na Utalii, Lazaro Nyalandu; Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi; William Lukuvi, Waziri wa Maji; Profesa Jumanne Maghembe na Waziri wa Kilimo, Chakula na Ushirika, Stephen Wasira.

Wakichangia taarifa ya utekelezaji wa shughuli za Kamati ya Kilimo, Mifugo na Maji na ile ya Ardhi, Maliasili na Mazingira, wabunge hao walionekana kukerwa na ahadi zisizotekelezeka za mawaziri hao kiasi cha wao kukata tamaa.

Mbunge wa Mwibara (CCM), Kangi Lugola akichangia taarifa hizo aliwashukia mawaziri watatu kwa wakati mmoja akieleza kuhusika kwao kukwamisha baadhi ya mambo.

Alisema migogoro ya ardhi nchini haitakwisha kama viongozi ndiyo wanaohusika kulinda baadhi ya watu. “Wako viongozi wanahodhi ardhi na kusababisha matatizo, mwekezaji wa Oysterbay Villa, Lukuvi ndiye alimsaidia kupata eneo alipokuwa Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam,” alisema Lugola na kuongeza:

“Sasa leo amekuwa Waziri wa Ardhi, itakuwaje? Mimi nitaichoma moto mbeleko inayombebea huyu mwekezaji kitendo kinachozuia Kinondoni kupata Sh3 bilioni. Huyu mwekezaji ana kiburi alizuia hata kamati kutaka kuingia kwenye eneo hilo lakini nikatumia ubaunsa wangu tukaingia.”

Hata hivyo, hoja ya Lugola kuhusu Lukuvi na mwekezaji huyo ilipingwa na Mbunge wa Kigoma Kaskazini (Chadema), Zitto Kabwe ambaye alisema waziri huyo alisaidia hata kubadilisha mkataba wa umiliki wa Oystebay Villa, hivyo amwache.

Lugola akiendelea kuchangia alimshukia Waziri Maghembe kwamba anapeleka maji katika eneo lake tu wakati wananchi wa jimbo la Mwibara na Bunda wakiteseka kwa mradi wao wa maji kutokukamilika.

“Waziri alisema uongo hapa kwamba mradi umekamilika kumbe ni uongo, niliwahi kuomba Rais atoe hawa mawaziri mizigo na nimefurahi amefanya mabadiliko hivyo naomba yawe ya tija,” alisema na kuongeza: “CCM isipigiwe kura hata mimi wasinipigie kama mradi wa maji hautakamilika.”

Kuhusu Kilimo alieleza kuwa wanailinda Bodi ya Pamba na ndiyo maana kuna uchakachuaji mkubwa wa mbegu za pamba.

Alimtaka Nyalandu kwenda Mwibara kufanya mkutano na mamba na viboko ambao wanakula wapigakura wake huku akikaa kimya.

“Lazaro Nyalandu uende ukawazuie mamba na viboko na kama unataka kwenda Ikulu halafu umeshindwa kuzuia mamba je, ukiwa Ikulu utaweza kweli? alihoji Lugola.

Akichangia hoja hiyo, Mbunge wa Kwela (CCM), Ignas Malocha aliwashukia Nyalandu na Profesa Maghembe kwa kutoa ahadi ambazo wameshindwa kutekelezeka.
Alisema ameshalalamikia suala la mamba katika jimbo lake lakini waziri amedanganya zaidi ya mara tatu bungeni.
“Nimeshazungumza hili suala la mamba hadi nimechoka, waziri anadanganya zaidi ya mara tatu na ameshindwa kutatua tatizo la mamba,” alisema Malocha huku akisema haiwezekani waziri akawa anasema uongo.
Alimgeukia Profesa Maghembe akieleza kuwa ni lazima aseme ni lini mradi wa maji katika Jimbo la Kwela na Sumbawanga kwa ujumla utakamilika...“Utuambie suala la maji mmefikia wapi mbona mnatudanganya?”
Kwa upande wake, Zitto alimweka Nyalandu kwenye wakati mgumu pale alipomwambia kuwa kama hatatoa tangazo la Serikali kuhusu kuanza kutumika kwa tozo mpya za Tanapa katika hoteli zilizopo katika hifadhi zake, basi awasilishe barua ya kujiuzulu kwa Rais kwa kuwa ameisababishia Serikali hasara ya Sh80 bilioni.
Taarifa ya Kamati ya Ardhi, Maliasili na Mazingira ilieleza kuwa Wizara ya Maliasili na Utalii haijatekeleza hukumu iliyotolewa na Mahakama Kuu Kanda ya Arusha iliyotaka wizara kutoa tangazo la kuanza kutumika kwa tozo mpya.
Taarifa hiyo iliyosomwa na Mwenyekiti wa kamati hiyo, James Lembeli imeeleza kuwa ni miezi minne sasa tangu hukumu hiyo itolewe lakini wizara haijatekeleza na kusababisha kupotea kwa Sh2 bilioni kila siku.
Akizungumzia taarifa hiyo, Zitto alisema anashangazwa kuwa waziri yupo halafu anashindwa kutekeleza agizo na akalitaka Bunge lichukue hatua.

 Zitto alishangazwa pia na taarifa ya kamati kutokutoa maagizo ya kufanya bali kushauri tu, jambo ambalo alisema lina walakini huku akihusisha jambo hilo na ushirikiano wa pacha watatu yaani Nyalandu, Lembeli na Mbunge wa Iringa Mjini, Peter Msigwa ambaye ni Waziri Kivuli wa Maliasili na Utalii.
“Haiwezekani hapa kuna mapacha watatu, waziri, mwenyekiti na waziri kivuli. Itakapofika jioni kama hajatoa tangazo tusimuone humu bungeni, upeleke barua ya kujiuzulu kwa Rais,” alisema Zitto.

Akijibu hoja zilizotolewa na wabunge, Waziri Lukuvi alisema atapambana na tatizo la migogoro ya ardhi nchini na kusisitiza kuwa Serikali itachukua mashamba yote makubwa ambayo hayaendelezwi.

Pia, alijibu hoja ya mwekezaji wa Oysterbay Villa akisema katika siku 10 alizokaa katika wizara hiyo, ametatua mgogoro huo hajausababisha kama Lugola alivyodai.
“Hati ilikuwa inaonyesha ni miaka 99 hivyo mimi nikaishusha hadi miaka 47 hivyo Kinondoni wameruhusiwa kukagua appartiments zao,” alisema.
Kwa upande wake, Waziri Nyalandu alitumia muda wake kuelezea tatizo la tozo ambalo wabunge wamelimlaumu akieleza kuwa kiasi cha Sh80 bilioni ambacho kinalalamikiwa ni cha miaka minane ambayo kesi ilikuwa mahakamani.
Alisema hata mahakama iliyotoa hukumu iliwashangaa wanasheria wa Tanapa kwa kushindwa kuishauri Serikali kutoa tangazo hilo. Baada ya kubanwa baadaye, Nyalandu alisema tangazo hilo litakuwa limetolewa ifikapo Februari 15.
Akijibu hoja za Wizara ya Kilimo, Wasira alisema anayafahamu matatizo kilimo hivyo atayashughulikia.
 
Akijibu hoja ya Lugola alisema anayajua matatizo ya wakulima wa pamba hivyo ataitisha kikao cha wabunge wote wanaotoka maeneo yanayolimwa pamba ili kupanga mikakati ya kushughulikia matatizo yaliyopo.
Profesa Maghembe alimshangaa Lugola kwa kutoa shutuma dhidi ya wizara yake wakati katika Jimbo la Mwibara limepatiwa miradi minne ya maji iliyokamilika na mitano inakaribia kumalizika ikiwa juu ya asilimia 50.
“Kama Lugola hayaoni haya basi naomba Spika mumsaidie apelekwe hospitali akapimwe,” alisema Profesa Maghembe.
Share on Google Plus

About Unknown

This is a short description in the author block about the author. You edit it by entering text in the "Biographical Info" field in the user admin panel.
    Blogger Comment
    Facebook Comment

0 comments:

Post a Comment