MAALIM SEIF KUKUTANA USO KWA USO NA HAMADI RASHID ZANZIBAR!!

Hamad Rashid (kushoto) Maalim Seif Sharif Hamad (kulia)
Mwanasiasa mkongwe nchini, Hamad Rashid Mohamed, atavaana na Katibu Mkuu wa Chama cha Wananchi (CUF), Maalim Seif Sharif Hamad katika kinyang’anyiro cha urais visiwani Zanzibar.
Hamad Rashid amekuwa mbunge wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa tiketi ya CUF kwa takriban miaka 20 sasa, lakini katika siku za hivi karibuni, alikwaruzana na chama hicho cha upinzani na kufukuzwa uanachama. Hata hivyo, alibakiwa na ubunge wake kutokana na amri ya Mahakama.
Katika mgogoro huo, Hamad Rashid alimtuhumu Seif ambaye ni Katibu Mkuu wa chama hicho kuwa alifanya makusudi kuvunja amri ya Mahakama iliyomtaka asitishe kikao kilichokuwa kikijadili hatima yake ndani ya chama hicho.
Maalim Seif ambaye pia ni Makamu wa Kwanza wa Rais wa Zanzibar, anatajwa kuwa ndiye atakayekuwa chaguo la Umoja wa Katiba ya Wananchi (Ukawa) kwa nafasi ya urais Zanzibar kutokana na CUF kuwa tayari imeshaota mizizi visiwani humo.
Hiyo itakuwa mara ya tano kwa Maalim Seif kugombea urais Zanzibar kama ataingia kwenye kinyang’anyiro hicho. Alianza kugombea nafasi hiyo mwaka 1995, akagombea tena 2000, kisha 2005 na mwaka 2010 na mara zote hizo, amekuwa akishindwa kwa tofauti ya kura chache na wagombea wa Chama cha Mapinduzi (CCM).
Kauli ya ADC
Naibu Katibu Mkuu wa Chama cha Alliance for Democratic Change (ADC), Doyo Hassan alisema jana kuwa kutokana na mgogoro uliopo na hasa Ukawa kuwa tayari wameshagawana majimbo, chama hicho kitasimamisha wagombea wake na Hamad Rashid ameshajitokeza kuutaka urais Zanzibar.
Alisema Hamad Rashid ameonyesha nia yake hiyo kwa viongozi wa chama na sasa anasubiri muda wa kuchukua fomu ili aanze mchakato huo wa kuitafuta Ikulu ya Zanzibar.
“(Hamad Rashid) anasubiri muda tu aje kuchukua fomu, lakini tayari amekuja tumezungumza naye na amekubali kuja kugombea urais kupitia chama chetu,” alisema Doyo ambaye alibainisha kuwa fomu hizo zitaanza kutolewa Julai Mosi hadi Julai 30 mwaka huu.
Hata hivyo, Doyo alitoa wito kwa wanachama wengine wa chama hicho kujitokeza kwa ajili ya kuwania nafasi hiyo ya juu ya uongozi wa nchi pamoja na nafasi za ubunge ili kuleta ushindani utakaokiwezesha chama kuwapata wagombea bora zaidi.
“Uchaguzi ndani ya chama kwa ajili ya kumpata mgombea urais, unatarajiwa kufanyika mara baada ya watia nia kurudisha fomu mwishoni mwa Julai na mgombea wetu atajulikana mwanzoni mwa Agosti,” alisema Doyo.
Mwananchi
Share on Google Plus

About Unknown

This is a short description in the author block about the author. You edit it by entering text in the "Biographical Info" field in the user admin panel.
    Blogger Comment
    Facebook Comment

0 comments:

Post a Comment