SERIKALI YALAUMIWA KUFUMBIA MACHO UKATILI WA KIJINSIA


IMEELEZWA kuwa maswala mengi yanayohusu ukatili wa Kijinsia yamekuwa yakifumbiwa macho na Serikali kwa kushindwa kuwachukuliwa hatua wahusika pindi wanapobainika kutenda makosa hayo hususani Jeshi la Polisi.
 
Hayo yalibainishwa mwishoni mwa Wiki katika Mafunzo ya waandishi wa habari juu ya kuandika habari za unyanyasaji wa kijinsia kwa Wanahabari wa Mikoa ya Rukwa na Katavi yaliyoandaliwa na Chama cha Wanahabari Wanawake Tanzania(TAMWA) yaliyofanyika katika ukumbi wa Hoteli ya Hollanda iliyopo mjini hapa.
 
 
Washiriki wa mafunzo hayo walisema pamoja na kazi ya Wanahabari kufanya kazi kama TAMWA inavyotaka ya kuibua matatizo ya ukatili wa kijinsia yanayofanyika vijijini lakini bado taasisi zinazotakiwa kuchukua hatua zaidi hazifanyi hivyo jambo linalokwamisha juhudi za waandishi wa habari.
 
Washiriki hao walitolea mfano wa kesi nyingi zinazoripotiwa na vyombo vya habari na jeshi kuwakamata wahusika na kuwaachia bila kutoa taarifa juu ya hatua zilizochukuliwa dhidi ya mhusika na badala yake mtuhumiwa kuendelea kutamba mitaani akijidai kushindwa kwa waliomshitaki.
 
Kwa upande wao wakufunzi wa Semina hiyo, Jamilah Kilahama na Ibrahimu Bakari kutoka TAMWA Dar Es Salaam, walisema moja ya sababu zinazofanya wahusika wa maswala ya unyanyasaji wa kijinsia kushindwa kuchukuliwa hatua ni pamoja na kujuana baina ya watenda makosa na Jeshi la polisi.
 
Waliongeza kuwa rushwa ni moja ya sababu ya kushindwa kukomeshwa kwa ukatili wa kijinsia kutokana na wahusika kutoa rushwa kwa vyombo vya dola pindi wanapo bainika kuhusika na uvunjifu wa haki za binadamu hasa kumtendea ndivyo sivyo mtoto na Mwanamke kwa kuwa ndiyo waathirika wakubwa wa unyanyasaji wa kijinsia.
 
Mbali na hilo walisema uoga uliojengeka ndani ya jamii ya kushindwa kuwashtaki watu wanaowabaini kuwatendea unyama watu wengine kwa kuhofia uhai wao kutoka kwa wahusika pamoja na kutengwa katika jamii ni moja ya sababu zinazochangia kutokukomeshwa kwa ukatili wa kijinsia.
 
Aidha washiriki wengi walilitupia lawama jeshi la polisi kwa kuendelea kuyafumbia macho maswala ya ukatili wa kijinsia ikiwa ni pamoja na wao kuendeleza ukatili huo kwa kuwatendea ndivyo sivyo baadhi ya watuhumiwa wanaofikishwa katika Vituo vyao wakitolea mfano Askari wa kiume kumpekua mtuhumiwa wa kike kuwa ni kinyume cha Sheria na haki za binadamu.
 
Wawezeshaji wa Semina hiyo walisema ni vema jamii ikaelewa Aina mbalimbali za ukatili wa Kijinsia kama ulivyoainishwa katika Miongozo ya TAMWA ili iweze kuyaepuka na kuyatolea ufumbuzi wa haraka pindi yanapotokea katika jamii zao.
 
Walizitaja aina hizo kuwa ni pamoja na ukatili wa kihisia na kisaikolojia, Mila na Desturi potofu, Ukatili wa Kimwili, Ukatili wa Kingono na ukatili wa kiuchumi ambao asilimia kubwa humwathiri mtoto na Mwanamke ambapo takwimu zinaonesha katika kila wanawake watano mmoja amepatwa na unyanyasaji na anatarajiwa kupata unyanyasaji wa kijinsia.
 
Hata hivyo Chama cha Wanahabari Wanawake Tanzania (TAMWA) kimejiwekea mpango mkakati wake wa miaka mitano 2000-2014, pamoja na mambo mengine kimepanga kufanya shughuli ambazo zitaimarisha elimu kwa mtoto wa kike kwa kupunguza vitendo vya ukatili wa kijinsia hasa vile vinavyoathiri wanawake na watoto. Vitendo hivyo ni pamoja na ubakaji, kulazimisha watoto wa kike kukatisha masomo na kuolewa, ukeketaji na familia kutelekeza watoto ambavyo kwa pamoja vinamnyima mtoto wa kike haki yake ya msingi ya kupata elimu.
Share on Google Plus

About Unknown

This is a short description in the author block about the author. You edit it by entering text in the "Biographical Info" field in the user admin panel.
    Blogger Comment
    Facebook Comment

0 comments:

Post a Comment