NJIA ZA KUREJESHA MABILIONI YA USWISI ZABAINIKA!!




Balozi wa Uswisi nchini, Olivier Chave alisema njia kuu na rahisi ya kuiwezesha Tanzania kurejesha fedha zake ni kujiunga na Shirika la Uchumi na Maendeleo (OECD) linalotatua matatizo ya uchumi, jamii na utawala.
“Tunachoweza kuwasaidia, kwa kawaida ni ushirikiano wa kodi ambapo nchi zinakubaliana na sheria za kimataifa na makubaliano. Sheria hiyo na kanuni zinafanya kazi chini ya OECD),” alisema Chave.
Dk Herkenrath alisema urejeshaji wa fedha zilizofichwa Uswisi hutegemea njia zilizotumika katika utoroshaji.
“Kwa fedha halali lakini hazikupitia mkondo sahihi hiyo ni rahisi kwani inahitaji makubaliano ya nchi mbili tofauti. Hadi sasa hakuna nchi ya Afrika iliyofanya makubaliano na Uswisi katika masuala ya ukwepaji wa kodi.”
Hata hivyo, alisema kwa ufahamu wake ni kwamba kwa kiasi kikubwa fedha za Tanzania zilizofichwa nchini humo zimepatikana kwa njia haramu ikiwa pamoja na rushwa. OECD iliyoanzishwa mwaka 1960 hadi sasa ina wanachama 34, lakini hadi sasa hakuna nchi ya Afrika iliyojiunga.
Naibu Waziri wa Fedha, Mwigulu Nchemba akizungumza jana alisema, “Kwetu sisi ikiwa taasisi yoyote inaweza kutusaidia kupata fedha ambazo zimefichwa huko, Serikali haina kipingamizi chochote cha kujiunga nayo.”
Hata hivyo, alisema hana uhakika iwapo mchakato wa kujinga na OECD umeanza. “Sina hakika sana na hilo ila ninavyofahamu kujiunga na taasisi zozote za kimataifa pia huwa kuna mambo mengi ya kuangalia, kama vile masharti yake, viwango vya ada maana siyo vizuri kujiunga na taasisi kama hizi halafu mkashindwa hata kulipa ada zinazotakiwa.”
Akizungumza katika mkutano na wahariri, Meneja wa Kitengo cha Kodi za Kimataifa cha Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA), Charles Bajungu alisema OECD ni taasisi inayozisaidia nchi nyingi za Ulaya kukabiliana na ukwepaji wa kodi.
Mmoja wa maofisa waandamizi katika Wizara ya Fedha ambaye aliomba jina lake lisitajwe alisema ikiwa Tanzania inataka kufanikiwa katika vita dhidi ya rushwa hasa utoroshaji wa fedha nje lazima iweke wazi taarifa zote za walipa kodi wakubwa.
“Lazima tujiunge na ‘Global Forum on Transparence and Exchange’. Huko taarifa zote za walipa kodi zinawekwa wazi. Ila Serikali yetu bado inasuasua, tumeshaishauri sana wizara lakini kuna urasimu fulani,” alisema.
Tayari Tanzania imeomba msaada kwa taasisi iitwayo International Centre for Asset Recovery (ICAR) (Kituo cha Kimataifa cha Urejeshaji wa Mali) ya Uswisi kuchunguza kesi tano zinazohusu watu na taasisi zinazotuhumiwa kuficha mabilioni ya fedha nchini humo.
Share on Google Plus

About Unknown

This is a short description in the author block about the author. You edit it by entering text in the "Biographical Info" field in the user admin panel.
    Blogger Comment
    Facebook Comment

0 comments:

Post a Comment