SAMWELI SITTA NA MBOWE WAINGIA VITANI!!

Mwenyekiti wa Bunge maalum la Katiba Mh.Samweli Sitta

Wakati Bunge Maalumu la Katiba likiazimia kuzifanyia marekebisho kanuni zake ili kuwabana wajumbe wa Bunge hilo ambao ni wanachama wa Umoja wa Katiba ya Wananchi (Ukawa), viongozi wa kundi hilo wamesema hawatishwi na uamuzi huo na kwamba wataendelea kususia vikao hivyo.
Kikao kilichokuwa kiwe cha mashauriano kilichoitishwa juzi na Mwenyekiti wa Bunge Maalumu, Samuel Sitta kiliazimia kuzifanya marekebisho baadhi kanuni za uendeshaji kwa lengo la kusimamia nidhamu wajumbe wake, hatua inayotafsiriwa kwamba inawalenga Ukawa.
Jana Sitta akizungumza na Mwananchi Jumamosi alisema mabadiliko yanayokusudiwa kufanywa yatahusisha masuala ya nidhamu, yakiwamo fujo na utoro, mambo ambayo hivi sasa hayawezi kudhibitiwa moja kwa moja na mwenyekiti wa Bunge hilo.
Sitta alikuwa akitoa ufafanuzi wa taarifa iliyotolewa na ofisi yake jana na kusomwa mbele ya waandishi wa habari na Katibu wa Bunge Maalumu, Yahya Khamis Hamad, ikieleza maazimio ya kikao ya usuluhishi alichokuwa amekiitisha kwa ajili ya kutanzua mzozo unaotishia kukwama kwa mchakato wa Katiba Mpya.
Hata hivyo, Ukawa unaoundwa na wajumbe wa Bunge Maalumu kutoka Vyama vya Chadema, NCCR Mageuzi, CUF na baadhi ya wajumbe kutoka Kundi la 201 walioteuliwa na Rais, walisusia kikao hicho na kusababisha uamuzi uliofikiwa kuwa wa upande mmoja.
Hata hivyo, wakizungumza na chanzo hiki jana kwa nyakati tofauti, viongozi wa Ukawa ambao ni Mwenyekiti wa Chadema, Freeman Mbowe na yule CUF, Profesa Ibrahim Lipumba walisema hawatishwi na mabadiliko ya kanuni yanayokusudiwa kufanywa na kwamba wataendelea kususia vikao hivyo hadi hoja zao zitakapozingatiwa.
Ukawa walitoka bungeni siku chache kabla ya kuahirishwa kwa awamu ya kwanza ya Bunge Maalumu mwezi Aprili mwaka huu, kwa madai kwamba Chama Cha Mapinduzi (CCM) kinatumia wingi wa wajumbe wake kutaka kufutwa kwa baadhi ya mapendekezo ya wananchi yaliyomo kwenye Rasimu ya Katiba.
Kauli ya Sitta
Sitta aliliambia gazeti hili kuwa moja ya kasoro katika uendeshaji wa Bunge ni pale makundi kama Ukawa na Tanzania Kwanza yanapotambuliwa kama makundi rasmi ya Bunge Maalumu, wakati makundi rasmi ni wabunge, wawakilishi na Kundi la Wajumbe 201 wa kuteuliwa na Rais.
“Bunge hili lina uhuru wa ajabu ambao ni mkubwa kuliko Bunge jingine lolote, Bunge ambalo hata uongozi wake hauwezi kumchukulia mtu hatua kwa utovu wa nidhamu eti mpaka umuone mtu anafanya makosa, umpeleke kwenye Kamati ya Kanuni na hivyo ndiyo inakuwa imekwisha maana kama ana watetezi wake wanamtetea,” alisema Sitta na kuongeza:
“Matokeo yake wananchi wanalalamika kwamba hakuna nidhamu bungeni na kwamba kiti kimeshindwa kuchukua hatua, sasa unachukuaje hatua wakati kanuni zetu ndivyo zilivyo?”
Aliendelea: “Yako mambo mengi yanapaswa kufanyika na tuna siku 63 tu za kukamilisha kazi tuliyopewa sasa hatuwezi kutumia fedha za umma na watu wengine wanafanya mzaha, leo huyu anachukua posho, mara anaondoka, haya mambo lazima yatafutiwe dawa.”
Source:Mwananchi.


Share on Google Plus

About Unknown

This is a short description in the author block about the author. You edit it by entering text in the "Biographical Info" field in the user admin panel.
    Blogger Comment
    Facebook Comment

0 comments:

Post a Comment