
Na Benedict Liwenga, Maelezo-Dodoma.
Katiba ni 
‘Sheria Mama’ inayolinda haki za raia wote wakiwemo wanawake, wanaume na
 watoto nchini na kuainisha mfumo wa kuendesha nchi na wajibu wa 
viongozi wanaopewa dhamana ya kuongoza.
Hivyo, ni 
vema Sheria hii Mama ikaheshimika na kila raia hasa pale inapokuwa 
ikiandaliwa ama kutungwa ili kuweza kupata Katiba rafiki yenye kumjali 
kila mwananchi kwa lengo la kudumisha maendeleo yenye tija katika taifa 
letu.
Hivi 
karibuni tumeshuhudia makundi mbalimbali yakiwasilisha nyongeza ya 
mapendekezo yao ya ziada katika Bunge Maalum la Katiba si kweli kama 
inavyodaiwa baadhi ya watu na vyombo vya habari, kuwa makundi hayo 
yalikuyanawasilisha hoja mpya, bali makundi haya yamekuwa yakidai kuwa 
baadhi ya mambo muhimu yalikuwa yamesahaulika au kutotiliwa mkazo wakati
 wa kukusanya maoni.
Kazi 
ambayo ilikuwa ikifanywa na Tume ya Marekebisho ya Katiba pindi 
walipowasilisha hoja zao hapo awali, ndipo wanapotumia wasaa huo 
kuwasilisha nyongeza ya mapendekezo hayo katika Bunge hilo.
Bila shaka
 kwa kitendo hiko wafanyacho waungwana hawa toka makundi mbalimbali ya 
wananchi si dhambi kwani wana nia nzuri ya kutaka kupata Katiba 
iliyorafiki na yenye mrengo wa kijinsia ili iweze kuwalinda na kuwaletea
 maendeleo katika taifa lao yaani Tanzania.
Mwenyekiti
 wa Bunge Maalum la Katiba, Mhe. Samuel Sitta amekuwa akisisitiza juu ya
 kazi yake anayoifanya katika Bunge hilo kuwa si kupokea hoja mpya na 
sio kufanya kazi ya iliyokuwa Tume ya Mabadiliko ya Katiba na ukweli huu
 unajidhihirisha pale alipofanya mikutano na baadhi ya makundi 
mbalimbali yaliyowahi kufika Bungeni hapo yakiwemo makundi ya Wasanii, 
Wafugaji, Wavuvi, Walemavu pamoja na Umoja wa Azaki za Vijana ambayo 
yaliwasilisha taarifa ya mapendekezo yao ikiwa ni nyongeza ya yale 
waliyokwisha wahi kuyawasilisha hapo awali ili yapate kuongezewa katika 
mchakato wa kusaka Katiba mpya.
Mwenyekiti
 wa Bunge hilo, Mhe. Sitta wakati alipokutana na kundi la Shirikisho la 
Vyama vya Watu wenye Ulemavu (SHIVYAWATA) alipata kutoa msisitizo wake 
kuhusiana na kazi ya Bunge hilo, huku akisisitiza kuwa kazi wanayoifanya
 ya kuyapokea makundi mbalimbali Bungeni hapo haina lengo la kuja na 
hoja mpya na kuziwasilisha katika Bunge hilo, bali ni mawasiliano ya 
kawaida yanayohusu safari kutoka Rasimu Mpya ya Katiba mpaka kufikia 
katika Katiba Mpya inayopendekezwa ipatikane.
Kauli 
ambayo amekuwa akiirudia mara kwa mara pindi anapokutana na makundi hayo
 wakiwemo baadhi ya waandishi wa habari ambao wanaripoti  habari za 
Bunge hilo.
“Jambo 
lolote lililoandikwa na binadamu halikosi kasoro, katika Rasimu hii ya 
Katiba tumegundua inayomapungufu kadha wa kadha, kuna baadhi ya maoni 
ambayo hayakuzingatiwa ndiyo maana tunayafanyia kazi ili yawemo katika 
Katiba Mpya itakayopatikana,”.alisema Mhe. Sitta.
Katika 
mchakato wa kusaka Katiba mpya, yatupasa kufahamu kuwa si Watanzania 
wote wenye nia nzuri ya kufanikisha suala hili liendelee vema kama 
ilivyopangwa, kwani kuna makundi mbalimbali wakiwemo watu binafsi wenye 
kujawa na chuki na sababu zisizo na mashiko na wenye lengo la 
kuwapotosha wananchi kuhusiana na mchakato huu wa kusaka Katiba mpya.
 Na ndiyo 
watu hawa tunapaswa tuwaelimisheili wapate kuelimika juu ya umuhimu wa 
Katiba hiyo kwani kuipinga, kuisema vibaya, kuidharau ikiwemo kuisusia 
pamoja na kudhalilisha wajumbe wa Bunge Maalum la Katiba wala hakuleti 
muafaka wowote kwakuwa Katiba hii itamfaa kila aliye Mtanzania hata huyu
 anayeipinga sasa kuwa mchakato wake usitishwe ama usiendelee.
Sambamba 
na haya, mnamo tarehe 3 Septemba mwaka huu,wawakilishi wa Taasisi za 
Dini wa Bunge Maalum la Katiba toka wajumbe 201 walitoa tamko lao dhidi 
ya tuhuma mbalimbali zinazoendelea katika kulichafua Bunge hilo, ikiwemo
 baadhi ya wajumbe wa kundi hilo wakituhumiwa kudaiwa kupewa rushwa.
Katika 
mkutano wao huo, tamko hilo lilitolewa na viongozi wa kiroho akiwemo 
Askofu wa Kikristo Amos Joseph Muhagachi pamoja na Sheikh Hamid Masoud 
Jongo wakiwa wameongozana na Mwenyekiti wa kundi hilo la 201, Mhe. Dkt. 
Francis Michael na wajumbe wengine wa kundi hilo, wakati walipofanya 
mkutano na waandishi wa habari kwenye Ukumbi wa Spika uliopo Bungeni 
mjini Dodoma.
Akisoma 
tamko hilo, Askofu Amos Muhagachi ambaye pia ni Mjumbe wa kundi hilo 
alisema kuwa kama ilivyoelezwa hapo awali kabla ya kuanza kwa shughuli 
za Bunge hilo, kila mjumbe alikula kiapo cha kuwa mwaminifu na mtiifu 
kwa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na kwa kadiri ya uwezo wake na 
ufahamu wake, kufanya kazi zinazomhusu bila upendeleo.
Askofu 
Muhagachi alieendelea kusema kuwa wameshangazwa na kusikitishwa kuona 
kwamba mchakato wa kutayarisha Katiba itakayopendekezwa na Bunge hilo 
kwa wananchi unachafuliwa taswira yake, Bunge Maalum la Katiba 
linachafuliwa, shughuli zake kuingiliwa na kupotoshwa na wajumbe wenzao 
walioko nje ya Bunge hilo, makundi, taasisi na vyombo mbalimbali vya 
habari.
Aliongeza kwamba, uhalali na ukweli wa shughuli za Bunge hilo unapotoshwa na wananchi wanaaminishwa mambo yasiyo na ukweli.
“Upotoshwaji huu umezua mijadala mbalimbali katika jamii ya Watanzania  nabado unaendelezwa”, alisema Muhagachi.
Aidha, Askofu Muhagachi alizitaja baadhi ya tuhuma zinazotolewa na wajumbe wenzao dhidi ya Bunge hilo zikiwemo;-
“Bunge 
Maalum la Katiba halina uhalali kwa kuwa hao wajumbe wenzetu walioondoka
 wameliondolea uhalali wake kwa vile hawapo, kwamba Kanuni za Bunge 
Maalum la Katiba zinavunjwa ovyo ovyo, Kwamba kinachojadiliwa sasa 
katika Bunge hili ni Waraka mwingine na si Rasimu iliyotayarishwa na 
Tume ya Mabadiliko ya Katiba, Inadaiwa na watu pamoja na Taasisi 
mbalimbali kwamba viongozi wa dini, wajumbe wa Bunge hilo na wajumbe wa 
kundi la 201 kwamba wanapewa rushwa baadhi ya Vyombo vya Habari 
vimeandika tuhuma hizi, pia madai mengine ni kwamba wajumbe waliomo 
katika Bunge hili ni wachache ikilinganishwa na hao waliopo nje ya Bunge
 na tuhuma ya nyingine ni ile ya kwamba Bunge hili lazima lisitishwe au 
livunjwe na Mhe. Rais.
“Tunapenda
 kuwafahamisha Watanzania wenzetu kwamba mchakato wa Katiba una hatua 
tatu kwa mujibu wa Sheria ya Mabadiliko ya Katiba na mpaka hivi sasa ni 
hatua moja iliyokamilika, aidha hatua ya pili ndiyo inayoendelea na 
hatua ya tatu bado haijaanza”, alisema Muhagachi.
Alisema idadi ya wajumbe wanaohudhuri Bunge hilo, wako zaidi ya robo tatu kati ya wajumbe wote walioteuliwa.
Akitoa 
tamko hilo, Askofu Muhagachi alisema kuwa wao kama wawakilishi wa 
Taasisi za Dini, ambao kuuhubiri, kuutangaza na kuusimamia ukweli ni 
moja ya majukumu yao katika jamii, hivyo wameskitishwa na taarifa potofu
 zinazosambazwa kwa makusudi na makundi, taasisi na baadhi ya vyombo vya
 habari.
“Tukiwa
 kama wajumbe wa Bunge hili ambao tunafahamu kwa kina na tunaridhika na 
kila hatua ya mchakato huu, tuna wajibu wa kusahihisha upotofu huu 
unaoendeshwa kwa makusudi na hivi kuwaeleza Watanzania ukweli na hali 
halisi inayojiri hapa Bungeni, Watanzania msifadhaishwe na wala 
msibabaishwe, hali ni shwari, mchakato unaendelea kwa amani na 
utulivu”, alisisitiza Muhagachi.
Katika 
mkutano wao huo naye Sheikh Hamid Masoud Jongo aliviasa vyombo vya 
habari kutilia mkazo katika kutoa taarifa zilizosahihi ili mchakato wa 
Katiba uendelee kwa amani kwani nao ni moja ya kundi la watu 
inayowahusu.
“Vyombo
 vya habari vina nguvu ya kuhabarisha umma juu ya mambo mengi 
yanayoendelea nchini, ni vema tukishirikiana sote kwa pamoja ili 
kuhakikisha kuwa tunapata Katiba yetu kwani hata nyie Katiba hii 
inawahusu hasa katika kudai haki na uhuru wa vyombo vya habari”, alisema Sheikh Jongo.
Pia 
Mwenyekiti wa wajumbe wa Kundi hilo la 201, Mhe. Dkt. Francis Michael 
aliongezea kwa kukanusha suala la rushwa kwa wajumbe wake huku 
akisisitiza kuwa wajumbe wake katika kundi hilo ni watu wenye heshima 
zao hivyo madai hayo hayakuwa na ukweli wowote.
Watanzania
 hatunabudi kulibariki na kuliheshimu Bunge  Maalum la Katiba pamoja na 
kazi zake na viongozi wake, na pia ni vema sasa kila mmoja kutokana na 
imani ya dini yake kwa wakati wake kuiombea kwa Mwenyezi Mungu ili aweze
 kuepusha ubaya wowote ambao unaweza kuikosesha haki ya Watanzania wote 
ya kupata Katiba Mpya iliyo bora, pia yatupasa kuwa makini dhidi ya watu
 wasiolitakia mema Bunge hili huku wakisahau kuwa wao pia ni miongoni 
mwa watu watakaonufaika na Katiba hiyo na hata vizazi vyao vya baadaye. 
Mungu ibariki Afrika, Mungu ibariki Tanzania.
0 comments:
Post a Comment