TULIBARIKI NA KULIHESHIMU BUNGE MAALUM LA KATIBA, ILI KATIBA MPYA ILIYO BORA IWEZE KUPATIKANA!!

samuel_sitta
Na Benedict Liwenga, Maelezo-Dodoma.
 
Katiba ni ‘Sheria Mama’ inayolinda haki za raia wote wakiwemo wanawake, wanaume na watoto nchini na kuainisha mfumo wa kuendesha nchi na wajibu wa viongozi wanaopewa dhamana ya kuongoza.
 
Hivyo, ni vema Sheria hii Mama ikaheshimika na kila raia hasa pale inapokuwa ikiandaliwa ama kutungwa ili kuweza kupata Katiba rafiki yenye kumjali kila mwananchi kwa lengo la kudumisha maendeleo yenye tija katika taifa letu.
 
Hivi karibuni tumeshuhudia makundi mbalimbali yakiwasilisha nyongeza ya mapendekezo yao ya ziada katika Bunge Maalum la Katiba si kweli kama inavyodaiwa baadhi ya watu na vyombo vya habari, kuwa makundi hayo yalikuyanawasilisha hoja mpya, bali makundi haya yamekuwa yakidai kuwa baadhi ya mambo muhimu yalikuwa yamesahaulika au kutotiliwa mkazo wakati wa kukusanya maoni.
 
Kazi ambayo ilikuwa ikifanywa na Tume ya Marekebisho ya Katiba pindi walipowasilisha hoja zao hapo awali, ndipo wanapotumia wasaa huo kuwasilisha nyongeza ya mapendekezo hayo katika Bunge hilo.
 
Bila shaka kwa kitendo hiko wafanyacho waungwana hawa toka makundi mbalimbali ya wananchi si dhambi kwani wana nia nzuri ya kutaka kupata Katiba iliyorafiki na yenye mrengo wa kijinsia ili iweze kuwalinda na kuwaletea maendeleo katika taifa lao yaani Tanzania.
 
Mwenyekiti wa Bunge Maalum la Katiba, Mhe. Samuel Sitta amekuwa akisisitiza juu ya kazi yake anayoifanya katika Bunge hilo kuwa si kupokea hoja mpya na sio kufanya kazi ya iliyokuwa Tume ya Mabadiliko ya Katiba na ukweli huu unajidhihirisha pale alipofanya mikutano na baadhi ya makundi mbalimbali yaliyowahi kufika Bungeni hapo yakiwemo makundi ya Wasanii, Wafugaji, Wavuvi, Walemavu pamoja na Umoja wa Azaki za Vijana ambayo yaliwasilisha taarifa ya mapendekezo yao ikiwa ni nyongeza ya yale waliyokwisha wahi kuyawasilisha hapo awali ili yapate kuongezewa katika mchakato wa kusaka Katiba mpya.
 
Mwenyekiti wa Bunge hilo, Mhe. Sitta wakati alipokutana na kundi la Shirikisho la Vyama vya Watu wenye Ulemavu (SHIVYAWATA) alipata kutoa msisitizo wake kuhusiana na kazi ya Bunge hilo, huku akisisitiza kuwa kazi wanayoifanya ya kuyapokea makundi mbalimbali Bungeni hapo haina lengo la kuja na hoja mpya na kuziwasilisha katika Bunge hilo, bali ni mawasiliano ya kawaida yanayohusu safari kutoka Rasimu Mpya ya Katiba mpaka kufikia katika Katiba Mpya inayopendekezwa ipatikane.
 
Kauli ambayo amekuwa akiirudia mara kwa mara pindi anapokutana na makundi hayo wakiwemo baadhi ya waandishi wa habari ambao wanaripoti  habari za Bunge hilo.
 
“Jambo lolote lililoandikwa na binadamu halikosi kasoro, katika Rasimu hii ya Katiba tumegundua inayomapungufu kadha wa kadha, kuna baadhi ya maoni ambayo hayakuzingatiwa ndiyo maana tunayafanyia kazi ili yawemo katika Katiba Mpya itakayopatikana,”.alisema Mhe. Sitta.
 
Katika mchakato wa kusaka Katiba mpya, yatupasa kufahamu kuwa si Watanzania wote wenye nia nzuri ya kufanikisha suala hili liendelee vema kama ilivyopangwa, kwani kuna makundi mbalimbali wakiwemo watu binafsi wenye kujawa na chuki na sababu zisizo na mashiko na wenye lengo la kuwapotosha wananchi kuhusiana na mchakato huu wa kusaka Katiba mpya.
 
 Na ndiyo watu hawa tunapaswa tuwaelimisheili wapate kuelimika juu ya umuhimu wa Katiba hiyo kwani kuipinga, kuisema vibaya, kuidharau ikiwemo kuisusia pamoja na kudhalilisha wajumbe wa Bunge Maalum la Katiba wala hakuleti muafaka wowote kwakuwa Katiba hii itamfaa kila aliye Mtanzania hata huyu anayeipinga sasa kuwa mchakato wake usitishwe ama usiendelee.
 
Sambamba na haya, mnamo tarehe 3 Septemba mwaka huu,wawakilishi wa Taasisi za Dini wa Bunge Maalum la Katiba toka wajumbe 201 walitoa tamko lao dhidi ya tuhuma mbalimbali zinazoendelea katika kulichafua Bunge hilo, ikiwemo baadhi ya wajumbe wa kundi hilo wakituhumiwa kudaiwa kupewa rushwa.
 
Katika mkutano wao huo, tamko hilo lilitolewa na viongozi wa kiroho akiwemo Askofu wa Kikristo Amos Joseph Muhagachi pamoja na Sheikh Hamid Masoud Jongo wakiwa wameongozana na Mwenyekiti wa kundi hilo la 201, Mhe. Dkt. Francis Michael na wajumbe wengine wa kundi hilo, wakati walipofanya mkutano na waandishi wa habari kwenye Ukumbi wa Spika uliopo Bungeni mjini Dodoma.
 
Akisoma tamko hilo, Askofu Amos Muhagachi ambaye pia ni Mjumbe wa kundi hilo alisema kuwa kama ilivyoelezwa hapo awali kabla ya kuanza kwa shughuli za Bunge hilo, kila mjumbe alikula kiapo cha kuwa mwaminifu na mtiifu kwa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na kwa kadiri ya uwezo wake na ufahamu wake, kufanya kazi zinazomhusu bila upendeleo.
 
Askofu Muhagachi alieendelea kusema kuwa wameshangazwa na kusikitishwa kuona kwamba mchakato wa kutayarisha Katiba itakayopendekezwa na Bunge hilo kwa wananchi unachafuliwa taswira yake, Bunge Maalum la Katiba linachafuliwa, shughuli zake kuingiliwa na kupotoshwa na wajumbe wenzao walioko nje ya Bunge hilo, makundi, taasisi na vyombo mbalimbali vya habari.
 
Aliongeza kwamba, uhalali na ukweli wa shughuli za Bunge hilo unapotoshwa na wananchi wanaaminishwa mambo yasiyo na ukweli.
 
“Upotoshwaji huu umezua mijadala mbalimbali katika jamii ya Watanzania  nabado unaendelezwa”, alisema Muhagachi.
 
Aidha, Askofu Muhagachi alizitaja baadhi ya tuhuma zinazotolewa na wajumbe wenzao dhidi ya Bunge hilo zikiwemo;-
 
“Bunge Maalum la Katiba halina uhalali kwa kuwa hao wajumbe wenzetu walioondoka wameliondolea uhalali wake kwa vile hawapo, kwamba Kanuni za Bunge Maalum la Katiba zinavunjwa ovyo ovyo, Kwamba kinachojadiliwa sasa katika Bunge hili ni Waraka mwingine na si Rasimu iliyotayarishwa na Tume ya Mabadiliko ya Katiba, Inadaiwa na watu pamoja na Taasisi mbalimbali kwamba viongozi wa dini, wajumbe wa Bunge hilo na wajumbe wa kundi la 201 kwamba wanapewa rushwa baadhi ya Vyombo vya Habari vimeandika tuhuma hizi, pia madai mengine ni kwamba wajumbe waliomo katika Bunge hili ni wachache ikilinganishwa na hao waliopo nje ya Bunge na tuhuma ya nyingine ni ile ya kwamba Bunge hili lazima lisitishwe au livunjwe na Mhe. Rais.
“Tunapenda kuwafahamisha Watanzania wenzetu kwamba mchakato wa Katiba una hatua tatu kwa mujibu wa Sheria ya Mabadiliko ya Katiba na mpaka hivi sasa ni hatua moja iliyokamilika, aidha hatua ya pili ndiyo inayoendelea na hatua ya tatu bado haijaanza”, alisema Muhagachi.
 
Alisema idadi ya wajumbe wanaohudhuri Bunge hilo, wako zaidi ya robo tatu kati ya wajumbe wote walioteuliwa.
 
Akitoa tamko hilo, Askofu Muhagachi alisema kuwa wao kama wawakilishi wa Taasisi za Dini, ambao kuuhubiri, kuutangaza na kuusimamia ukweli ni moja ya majukumu yao katika jamii, hivyo wameskitishwa na taarifa potofu zinazosambazwa kwa makusudi na makundi, taasisi na baadhi ya vyombo vya habari.
 
“Tukiwa kama wajumbe wa Bunge hili ambao tunafahamu kwa kina na tunaridhika na kila hatua ya mchakato huu, tuna wajibu wa kusahihisha upotofu huu unaoendeshwa kwa makusudi na hivi kuwaeleza Watanzania ukweli na hali halisi inayojiri hapa Bungeni, Watanzania msifadhaishwe na wala msibabaishwe, hali ni shwari, mchakato unaendelea kwa amani na utulivu”, alisisitiza Muhagachi.
 
Katika mkutano wao huo naye Sheikh Hamid Masoud Jongo aliviasa vyombo vya habari kutilia mkazo katika kutoa taarifa zilizosahihi ili mchakato wa Katiba uendelee kwa amani kwani nao ni moja ya kundi la watu inayowahusu.
 
“Vyombo vya habari vina nguvu ya kuhabarisha umma juu ya mambo mengi yanayoendelea nchini, ni vema tukishirikiana sote kwa pamoja ili kuhakikisha kuwa tunapata Katiba yetu kwani hata nyie Katiba hii inawahusu hasa katika kudai haki na uhuru wa vyombo vya habari”, alisema Sheikh Jongo.
 
Pia Mwenyekiti wa wajumbe wa Kundi hilo la 201, Mhe. Dkt. Francis Michael aliongezea kwa kukanusha suala la rushwa kwa wajumbe wake huku akisisitiza kuwa wajumbe wake katika kundi hilo ni watu wenye heshima zao hivyo madai hayo hayakuwa na ukweli wowote.
 
Watanzania hatunabudi kulibariki na kuliheshimu Bunge  Maalum la Katiba pamoja na kazi zake na viongozi wake, na pia ni vema sasa kila mmoja kutokana na imani ya dini yake kwa wakati wake kuiombea kwa Mwenyezi Mungu ili aweze kuepusha ubaya wowote ambao unaweza kuikosesha haki ya Watanzania wote ya kupata Katiba Mpya iliyo bora, pia yatupasa kuwa makini dhidi ya watu wasiolitakia mema Bunge hili huku wakisahau kuwa wao pia ni miongoni mwa watu watakaonufaika na Katiba hiyo na hata vizazi vyao vya baadaye. Mungu ibariki Afrika, Mungu ibariki Tanzania.
Share on Google Plus

About Unknown

This is a short description in the author block about the author. You edit it by entering text in the "Biographical Info" field in the user admin panel.
    Blogger Comment
    Facebook Comment

0 comments:

Post a Comment