
Mbunge wa Kigoma Kaskazini, Zitto Kabwe akifafanua jambo.
Zitto (37), ambaye alikuwa naibu katibu mkuu wa 
Chadema, alisema kuwa hata kuvuliwa nyadhifa zake ndani ya chama 
kulisababishwa na wapambe hao, lakini akasisitiza kuwa hana kinyongo 
tena kwa kuwa alishamwomba Mungu na sasa amesamehe kabisa.
                
              
Tofauti za wawili hao hazijawahi kutolewa 
hadharani licha ya mitandao mbalimbali kuzungumzia kuharibika kwa 
uhusiano wao ikinukuu habari kutoka vikao vya ndani vya Chadema.
                
              
Hata hivyo, mapema mwaka huu, Zitto alirushiwa 
tuhuma nzito na Chadema kutokana na uhusiano wake na baadhi ya makada wa
 CCM, lakini mbunge huyo aliyahusisha maneno hayo na mwenyekiti wake na 
aliandika maneno makali dhidi ya Mbowe kwenye ukurasa wake wa facebook.
                
              
Lakini katika mahojiano na Mwananchi yaliyofanyika
 wiki iliyopita nyumbani kwake Masaki jijini Dar es Salaam, Zitto 
alionekana kujutia kuharibika huko kwa uhusiano wao na kusema “wapambe 
ndiyo wanatugombanisha”.
                
              
“Sina shida yoyote na Mbowe, naamini ipo siku 
tutagundua wapambe walituathiri na ndiyo waliotufikisha hapa,” 
alisisitiza Zitto bila kutaja ni kina nani hasa.
                
              
Zitto alisema yeye na Mbowe wametoka mbali tangu 
akiwa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam na hafurahii uhusiano wao ukiishia 
katika hali hiyo.
                
              
“Naumia sana, lakini naamini ipo siku ama nikiwa 
hai au nimekufa watu wataujua ukweli,” alisema mwanasiasa huyo kijana 
aliyepata umaarufu kutokana na uwezo wake wa kujenga hoja.
                
              
Alisema, akiwa mwenyekiti wa Serikali ya wanafunzi
 wa Chuo Kikuu (Daruso) yeye na mwenyekiti wake ndiyo waliokijenga chama
 wakati huo Mbowe akiwa mbunge wa Hai.
                
              
Alisema wakati huo Mbowe alikuwa akienda chumbani 
kwake kusuka mikakati ya kuiinua Chadema na kwamba walikuwa wakila chips
 pamoja na wakati mwingine kwenye klabu ya usiku ya Bilicanas 
inayomilikiwa na Mbowe.
                
              
“Wakati mwingine naangalia, naumia sana. Wakati 
tunafanya hayo yote wengine walikuwa CCM, wengine walikuwa 
wafanyabiashara, lakini sasa ndiyo wana sauti katika chama,” alisema 
Zitto.
                
              
Zitto alisema kuwa wakati huo walikuwa na kampeni 
yao waliyoiita ‘Real Madrid’ ambayo ilikuwa na lengo la kuingiza kila 
mwanasiasa bora katika chama chao.
0 comments:
Post a Comment