ZITO KABWE AJUTIA KUGOMBANA NA MBOWE!!



Mbunge wa Kigoma Kaskazini, Zitto Kabwe akifafanua jambo.
 Mbunge wa Kigoma Kaskazini, Zitto Kabwe ameeleza tofauti yake na mwenyekiti wa Chadema, Freeman Mbowe, akisema imesababishwa na watu aliowaita wapambe.
Zitto (37), ambaye alikuwa naibu katibu mkuu wa Chadema, alisema kuwa hata kuvuliwa nyadhifa zake ndani ya chama kulisababishwa na wapambe hao, lakini akasisitiza kuwa hana kinyongo tena kwa kuwa alishamwomba Mungu na sasa amesamehe kabisa.

Tofauti za wawili hao hazijawahi kutolewa hadharani licha ya mitandao mbalimbali kuzungumzia kuharibika kwa uhusiano wao ikinukuu habari kutoka vikao vya ndani vya Chadema.

Hata hivyo, mapema mwaka huu, Zitto alirushiwa tuhuma nzito na Chadema kutokana na uhusiano wake na baadhi ya makada wa CCM, lakini mbunge huyo aliyahusisha maneno hayo na mwenyekiti wake na aliandika maneno makali dhidi ya Mbowe kwenye ukurasa wake wa facebook.

Lakini katika mahojiano na Mwananchi yaliyofanyika wiki iliyopita nyumbani kwake Masaki jijini Dar es Salaam, Zitto alionekana kujutia kuharibika huko kwa uhusiano wao na kusema “wapambe ndiyo wanatugombanisha”.

“Sina shida yoyote na Mbowe, naamini ipo siku tutagundua wapambe walituathiri na ndiyo waliotufikisha hapa,” alisisitiza Zitto bila kutaja ni kina nani hasa.

Zitto alisema yeye na Mbowe wametoka mbali tangu akiwa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam na hafurahii uhusiano wao ukiishia katika hali hiyo.

“Naumia sana, lakini naamini ipo siku ama nikiwa hai au nimekufa watu wataujua ukweli,” alisema mwanasiasa huyo kijana aliyepata umaarufu kutokana na uwezo wake wa kujenga hoja.

Alisema, akiwa mwenyekiti wa Serikali ya wanafunzi wa Chuo Kikuu (Daruso) yeye na mwenyekiti wake ndiyo waliokijenga chama wakati huo Mbowe akiwa mbunge wa Hai.

Alisema wakati huo Mbowe alikuwa akienda chumbani kwake kusuka mikakati ya kuiinua Chadema na kwamba walikuwa wakila chips pamoja na wakati mwingine kwenye klabu ya usiku ya Bilicanas inayomilikiwa na Mbowe.

“Wakati mwingine naangalia, naumia sana. Wakati tunafanya hayo yote wengine walikuwa CCM, wengine walikuwa wafanyabiashara, lakini sasa ndiyo wana sauti katika chama,” alisema Zitto.

Zitto alisema kuwa wakati huo walikuwa na kampeni yao waliyoiita ‘Real Madrid’ ambayo ilikuwa na lengo la kuingiza kila mwanasiasa bora katika chama chao.
Share on Google Plus

About Unknown

This is a short description in the author block about the author. You edit it by entering text in the "Biographical Info" field in the user admin panel.
    Blogger Comment
    Facebook Comment

0 comments:

Post a Comment