KUELEKEA UCHAGUZI OCTOBER 2015;TATHIMINI 10 ZA MRITHI WA RAIS JAKAYA KIKWETE!!

Rais Jakaya Mrisho Kikwete (Picha na Maktaba)
Wakati mjadala wa majina ya watu wanaotaka kuwania urais umepamba moto, baadhi ya wasomi, wachambuzi na wasomaji wa gazeti hili wamesema badala ya kukimbilia majina, wagombea hao wanatakiwa kueleza jinsi gani watakavyokabiliana na ajenda 10 muhimu kwa maendeleo ya Taifa.
 
Ajenda hizo kwa mujibu wa wadau wa kada mbalimbali waliongelea kuhusu vipaumbele vya taifa kwa sasa, ni tatizo la ajira, changamoto za kuinua kilimo, kutoa elimu bora, kusimamia makusanyo ya kodi, rasilimali za taifa na kuboresha miundombinu ya usafiri.
Wagombea hao pia watatakiwa kueleza jinsi watakavyoondoa migogoro ya wakulima na wafugaji, matumizi sahihi ya ardhi, mapambano dhidi ya rushwa, uhalifu na matumizi ya dawa za kulevya, kwa mujibu wa marejeo ya habari mbalimbali yaliyofanywa na wachunguzi wetu.
Kwa kawaida, vyama vya siasa huandaa ilani zake za uchaguzi ambazo ndiyo mwongozo wa kampeni za kutafuta kura kwa wananchi kwa ajili ya wagombea wake wa urais, ubunge na udiwani, lakini watatakiwa kuzingatia hoja hizo muhimu.
Katika mahojiano na wadau mbalimbali, gazeti la Mwananchi lilitaka kujua ni mambo gani ambayo wananchi “wanataka yawe ajenda kuu kwenye kampeni za uchaguzi ili kuikwamua nchi” kutoka hapa ilipo, na majibu yao yalionyesha suala la ajira, kilimo, afya, rasilimali za taifa, usafiri, maji, rushwa na migogoro ya ardhi kuwa ndiyo mambo ambayo hayajafanyiwa kazi na hivyo wanataka kusikia wagombea watakavyokabiliana nayo.
“Kwanza tunahitaji utawala bora unaosimamia haki, Serikali inayofanya uamuzi sahihi,” alisema mwanasheria wa jijini Dar es Salaam, Felix Kibodya kabla ya kutaja mambo ambayo anaona yanafaa kupewa kipaumbele.
Usimamizi wa rasilimali
Kibodya, ambaye amewahi kuwa rais wa Chama cha Wanasheria wa Tanganyika (TLS), alisema rasilimali zikisimamiwa na kutumika vizuri, zitalinufaisha Taifa kwa kiasi kikubwa.
“Kuna viongozi katika nchi hii waliwahi kueleza wazi kwamba rasilimali zikibaki ardhini haziozi. Tukifanya mchezo rasilimali hizi zitakwisha. Suala hili linaenda sambamba na ubinafsishaji tulioufanya miaka ya nyuma, sasa ndiyo tunaaza kuona ubaya wake,” alisema.
Alikuwa akizungumzia rasilimali kama dhahabu, chuma, shaba, platinum, nickel, almasi, tanzanite, rubi, garnet, emerald, sapphire na maliasili nyingine kama gesi na mafuta.
Kati ya madini hayo, dhahabu na almasi ndiyo zimekuwa tegemeo kubwa kwa uchumi wa Tanzania, wakati kugundulika kwa gesi na uwezekano wa kupatikana kwa mafuta kumeinua matarajio ya maisha bora kwa wananchi na wakati fulani Rais Jakaya Kikwete aliwahi kunukuliwa akisema “atakuwa Rais wa mwisho kuiacha nchi maskini”.
Lakini kilio kikubwa cha wadau imekuwa ni mikataba, ambayo imeelezwa kuwa ni ya siri na hainufaishi Taifa na badala yake inanufaisha wawekezaji na wajanja wachache.


“Hatuna sababu ya kukopa kwa mataifa tajiri wakati tuna rasilimali za kutuingizia fedha nyingi. Tukiweza kusimamia vizuri vivutio vya utalii, gesi, mafuta na madini tutapiga hatua kubwa,” alisema mhadhiri wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam katika Idara ya Sayansi ya Siasa, Richard Mbunda.
Mbunda alitaja mambo matatu yanayotakiwa kusimamiwa kwa umakini kuwa ni matumizi bora ya rasilimali, miundombinu na kilimo.
Claudian Mutayoba mkazi wa Kigoma alisema: “Jambo la muhimu ninaloliona wazi kuwa linaweza kutusaidia ni rasilimali tulizonazo. Kama Serikali itaweka mikakati madhubuti ya kuzisimamia zinaweza kutufikisha mbali. Hilo halifanyiki na ndiyo maana madini yanaibwa na wanyama kusafirishwa nje ya nchi.”
Ajira
Tatizo la ajira limekuwa likizungumzwa na wengi, wakiwamo waliotangaza na wanaotajwa kuwania urais, wote wakielezea kuwa ni bomu linaloweza kuibuka wakati wote. Kwa sasa takriban watu milioni 21 ni nguvu kazi iliyoko sokoni na kati yao, milioni 6.5 tu ndiyo walio na ajira, wakati watu 800,000 hadi 1,000,000 wanaingia kwenye soko la ajira kila mwaka.
Idadi hiyo ya watu wanaostahili kuajiriwa ni kuanzia vijana wa miaka 15 ambao wakati wowote wanaingia sokoni kusaka ajira na kwa mujibu wa takwimu hizo za Ofisi ya Takwimu ya Taifa (NBS) za mwaka 2012, idadi ya walio tayari kwenye soko la ajira ni takriban nusu ya idadi ya Watanzania.
“Maendeleo yanatakiwa kusimamiwa. Nchi yetu ina tatizo kubwa la ardhi na ajira. Tunatakiwa kujiuliza sababu za wanakijiji na mwekezaji kugombania ardhi. Iweje mwekezaji apewe ardhi na mwananchi ahamishwe,” alisema Profesa Penina Mlama, ambaye ni mwenyekiti wa Kigoda cha Taaluma cha Mwalimu Nyerere.
“Tazama ajira. Ni tatizo kubwa ni vyema tukaweka utaratibu wa kila mwekezaji nchini kuajiri idadi fulani ya Watanzania, hiyo iwe lazima si ombi.”
Hoja hiyo iliungwa mkono na Tito Kisiya, mkazi wa jijini Dar es Salaam, ambaye alisema ajira ni ajenda namba moja.
“Kipaumbele namba moja ni ajira. Huwezi kukuza uchumi wa nchi kama rasilimali watu haitumiki inavyotakiwa. Pia, msisitizo mkubwa uwekwe katika viwanda kwa kujenga vipya, kufufua vilivyokuwapo ili kuchochea ukuaji wa uchumi wa nchi,” alisema akiungana na wengi waliozungumza na Mwananchi.
Desmund Mgongolwa pia alikuwa na maoni kama hayo aliposema: “Ajira zipewe kipaumbele. Kuna haja ya kuunda mfuko wa kukopesha vijana wasio na ajira ili waunde vikundi vya kufanya biashara.”
Kilimo
Suala la kuboresha kilimo ili kiwanufaishe wakulima pia lilikuwa midomoni mwa wengi na walisema kilimo sasa hakina usimamizi na hivyo kupoteza umuhimu wake.
Inakadiriwa kuwa zaidi ya asilimia 70 ya Watanzania wanaishi vijijini ambako kilimo kilikuwa kikielezewa kuwa ni uti wa mgongo wa uchumi, lakini katika siku za karibuni makundi ya vijana yamekuwa yakimiminika mijini na kujishughulisha na biashara ndogondogo kutokana na kilimo kuonekana kutokuwa na manufaa kiuchumi.
Kilimo kinachangia asilimia 27.8 ya Pato la Taifa kutokana na mazao ya pamba, kahawa, chai, tumbaku, katani na karanga wakati mazao ya chakula ni mahindi, maharage, viazi na mihogo.
Mhadhiri Mwandamizi wa Chuo Kikuu cha Ruaha, Profesa Gaudence Mpangala alizungumzia zaidi suala la kilimo akihusisha na dhana ya soko huria.
“Dhana ya soko huria ndiyo sababu ya kilimo kutowanufaisha wananchi na kutochangia Pato la Taifa kama inavyotakiwa,” alisema.
Akizungumzia mambo yanayotakiwa kuwa ajenda kuu katika uchaguzi alisema ajenda ya kwanza ni kukuza uchumi ambao ukuaji wake utatokana na kuboreshwa kwa sekta ya kilimo na viwanda.
“Jambo la pili ni kutokomeza umaskini ambalo litakwenda sambamba na kumaliza tatizo la ajira. Tatu ni kutokemeza ufisadi na rushwa na nne kujenga misingi imara ya demokrasia,” alisema.
“Serikali imejiondoa katika kusimamia na kudhibiti uchumi na hali hii inatokea karibu kila sekta nchini. Mfano, mapato ya wakulima ni madogo, hawana soko la kueleweka na hata likiwapo bado wanapangiwa bei za kuuza mazao yao,” alisema.
Alisema barani Afrika Tanzania ni kati ya nchi ambazo zinategemea jembe la mkono kwa kilimo, jambo ambalo haliwezekani kulikuta nchi nyingine zinazoendelea.
“Tuna sera ya kilimo kwanza lakini haijasaidia kuinua kilimo. Kilimo kikifanywa vizuri ni chanzo kizuri cha mapato na hata kuliletea Taifa letu maendeleo, zipo nchi nyingi duniani zimeendelea kwa sababu tu ya kilimo,” alisema.
Elimu
Wakati Serikali imezindua Sera ya Elimu bora, wadau wanaona kuwa bado Serikali ya Awamu ya Tano itatakiwa kufanya kazi kubwa kuboresha elimu.

“Mimi naona vipaumbele vikubwa mwaka huu viwe ni ajira, elimu bora inayozalisha vijana wanaojitegemea na usimamizi mzuri wa rasilimali,” alisema Dickson Kikoti, mtaalamu wa Sayansi ya Siasa.
Suala hilo pia lilizungumziwa na mhadhiri wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, Richard Mbunda ambaye alisema elimu ni moja ya ajenda kuu ambazo anadhani wagombea uongozi kwenye uchaguzi mkuu ujao wangetakiwa walizungumzie kwa kina.
“Ajenda zinatakiwa kutoka kwa mgombea mwenyewe, ila binafsi ukinitaka nitaje nitasisitiza zaidi suala la kuwa na msingi bora wa elimu ikiwa ni pamoja kuimarisha miundombinu yake, kuhakikisha kuwa kila Mtanzania anapata huduma bora ya afya,” alisema.
Miundombinu ya usafiri
Wakati Serikali ya Awamu ya Tatu imefanya kazi kubwa ya kuunganisha nchi kwa kutengeneza mtandao wa barabara, bado tatizo la usafiri wa reli kutorekebishwa linaonekana kuathiri wananchi wengi na kuathiri barabara zenyewe.
Tanzania ina mtandao wa barabara wa kilomita 86,472, wakati Wizara ya Ujenzi inasimamia barabara za urefu wa kilomita 33,891. Kati ya hizo, barabara za urefu wa kilomita 12,786 zinaunganisha mikoa na nyingine za urefu wa kilomita 21,105 za ndani ya mikoa.
Kwa mujibu wa tovuti ya Tanroads, kati ya barabara za urefu wa kilomita 12,786 ambazo hutumiwa na magari makubwa, ni kilomita 5,130 zilizojengwa.
“Huwezi kujenga barabara na kisha ukaacha kujenga reli. Ukifanya hivyo barabara unazojenga hazitadumu. Suala la kuwa na reli za kutosha ni muhimu lakini halipewi uzito wa kutosha,” alisema Kibodya.
Naye Christopher Bernard, mkazi wa Dar es Salaam ambaye amehitimu masomo ya shahada ya biashara mwaka jana, alizungumzia suala la miundombinu akitoa mfano wa bandari.
“Hapa kwetu tuna bandari, mito, maziwa, madini lakini tumeshindwa kuvitumia. Binafsi nadhani tunashindwa kutokana na kukosa utawala bora. Ila ukiniambia mambo gani ya msingi tunayotakiwa kufanya, nitakujibu kuwa ni kilimo, miundombinu na rasilimali,” alisema.
Mbunda aliongeza kuwa usafiri wa reli ndiyo utawakomboa wananchi kwa kupunguza gharama za usafiri na kuondoa misongamano ya magari isiyokuwa na sababu.
“Ukiwa na reli utasafirisha mizigo kwa urahisi, usalama na kwa muda mfupi na kuondoa msongamano usiyo na msingi. Nchi ikiwa ni miundombinu ya kutosha kila jambo litakwenda vizuri na uchumi utakuwa.”

Maji
Kwa mujibu wa marejeo mbalimbali ya habari kuhusu matatizo ya wananchi, suala la maji, ambalo limeingizwa kwenye Katiba Inayopendekezwa kama moja ya haki za msingi, bado ni tatizo kubwa na jitihada za kuanzisha miradi mbalimbali ya majisafi hazijawezesha huduma hiyo kufika kwa asilimia kubwa ya wananchi.
Kwa mujibu wa takwimu za NBS, ni asilimia 25 tu ya watu waishio vijijini ndiyo wanaopata maji ya bomba, wakati asilimia 18.4 wanapata maji safi kutoka vyanzo vingine na asilimia 56.7 haipati majisafi.
Kwa mujibu wa takwimu hizo, asilimia 57.9 ya watu waishio mijini wananufaika na maji ya bomba, wakati wengine 25.6 wanapata maji kutoka vyanzo vingine huku asilimia 16.5 ikikosa huduma hiyo muhimu. Mbali na maji safi, upatikanaji wa maji umekuwa ni tatizo kutokana na wananchi kulazimika kufuata umbali mrefu.
Kodi
Wananchi walioongea na gazeti hili pia walitaka ukusanyaji mbovu wa kodi kuwa ni moja ya matatizo na kutaka wagombea walieleza kwa kina jinsi watakavyolishughulikia.
Mmoja wa watu hao ni Mbunge wa Kibaha, Silvester Koka ambaye alisema kuwa anatamani kuona rais ajaye anasimamia ipasavyo kodi na suala zima la rasilimali za nchi.
Alisema uchumi wa Tanzania na maendeleo yake unategemea sana kodi ambayo kila mmoja atafaidi matunda yake.
“Haiwezekani watu wanakwepa kodi halafu wanataka maendeleo, kodi haikusanywi ipasavyo halafu tunataka maendeleo, hiyo haipo,” alisema.
Akizungumzia raslimali, alisema raslimali za Tanzania zinatosheleza Taifa, lakini usimamizi si madhubuti, hivyo, rais ajaye anatakiwa kuangalia kwa umakini maeneo hayo.
Mahakama ya Kadhi
Suala la Mahakama ya Kadhi limekuwa likizungumzwa tangu wakati wa kampeni za urais za mwaka 2005 na CCM ililiweka kwenye ilani yake ikiahidi kuwa ingelishughulikia, lakini hadi leo bado halijapatiwa ufumbuzi.


Muswada uliolenga kuifanya Mahakama ya Kadhi itambuliwe ambao ulitakiwa uwasilishwe kwenye mkutano uliopita wa Bunge, ulikwama baada ya kuwa na kasoro nyingi na Waziri Mkuu Mizengo Pinda alisema muswada huo umeondolewa ili kutoa nafasi zaidi ya watu kujadili.
Wakizungumzia Mahakama ya Kadhi wananchi hao walisema kuwa suala hilo ni haki za msingi na hivyo linapaswa kushughulikiwa ili kuwapa wanaohitaji haki yao ya kikatiba, huku wengine wakisema suala hilo halitakiwi kuwamo kwenye katiba.
Mijadala kuhusu suala hilo ambayo imekuwapo inaonyesha bila ya kushughulikiwa, linaweza kuwagawa watu, kama ilivyokuwa kwenye kashfa ya uchotwaji fedha kwenye Akaunti ya Tegeta Escrow ambalo walisema liliwagawa watu kutokana na kundi moja kuona jingine linafaidi zaidi.
Dawa za kulevya
Pia, tangu Serikali ya Awamu ya Nne iingie madarakani imekuwa ikiahidi kushughulikia tatizo la dawa za kulevya, lakini bado Dar es Salaam na Zanzibar zimeendelea kuwa vituo vikuu vya kupitishia dawa hizo zilizoharamishwa kimataifa.
Fedha nyingi zitokanazo na dawa hizo zimekuwa zikihusishwa na kukua kwa vitendo vya ugaidi, wakati matumizi ya dawa hizo yanaathiri afya, hasa za vijana ambao ni taifa la kesho.
Migogoro ya ardhi
Kati ya maeneo ambayo hayajapata ufumbuzi ni suala la migogoro ya ardhi karibu maeneo mbalimbali ya nchi.
Kukithiri kwa migogoro hiyo, kulimlazimisha Spika wa Bunge, Anne Makinda kuunda Kamati maalumu ya Bunge chini ya Mwenyekiti wake, Christopher Ole Sendeka kuchunguza chanzo chake hasa kwa wakulima, wafugaji, wawekezaji na watumiaji wengine wa ardhi nchini.
Rais ajaye anatakiwa kuangalia maeneo yenye migogoro; Kiteto (Manyara), Morogoro maeneo ya Kilosa, Ifakara na Mahenge.
Maeneo mengine yenye migogoro ni; Mwanza na Mara.
 CHANZO: Mwananchi
Share on Google Plus

About Unknown

This is a short description in the author block about the author. You edit it by entering text in the "Biographical Info" field in the user admin panel.
    Blogger Comment
    Facebook Comment

0 comments:

Post a Comment