WANANCHI WASIFIA MFUMO WA BVR!!

Mtaalamu wa Mashine ya Biometrick Voters Registration (BVR), Typhone Lumato akichukua maelezo kwa mkazi wa Mtaa wa Lumumba, Makambako mkoani Njombe, Ephaimu Matandala wakati akimwandikisha katika Daftari la Kudumu la Wapigakura, jana.
Kazi ya kuandikisha wananchi katika Daftari la Kudumu la Wapigakura kupitia mfumo wa Biometrick Voters Registration (BVR), ambao huhusisha uchukuaji wa alama za vidole na picha, jana iliingia siku ya tatu, huku baadhi yao wakipongeza utendaji wake.

Wakizungumza na waandishi wa habari kwa nyakati tofauti mjini hapa katika vituo vya uandikishaji, wananchi hao walisema kuna mabadiliko ukilinganisha na siku zilizopita, hivi sasa kazi zinafanywa haraka.
Mmoja wa waliojiandikisha katika daftari hilo, Nico Ndembe alisema idadi ya watu wanaokwenda katika vituo ni kubwa, hivyo wanatakiwa kuongeza mashine au muda wa kujiandikisha.
“Natoa ushauri kwa wataalamu wa tume kama wanaweza kutambua uwezo wa mashine zinaandikisha idadi ya watu kiasi gani kwa siku, jambo muhimu kwao ni kuandika namba za watu wanaopaswa kuandikishwa, kisha wanaozidi wanarudi nyumbani,” alisema Ndembe.
Alisema hiyo itasaidia wale wanaosubiri muda muda mrefu bila kupata huduma, waendelee kufanya shughuli zao nyingine.
Naye, Aldol Mchapa alisema awali kazi hiyo ilikuwa ikichukua muda mrefu, lakini hivi sasa inachukua muda mfupi.
Katibu wa Chadema, Jimbo la Njombe, David Tweve alisema mabadiliko yapo katika vituo mbalimbali, lakini muda uliopangwa hautoshi.
Tweve alitoa mfano katika Kituo cha Lupila kwamba watu waliojiorodhesha kwenye kituo hicho ili wapate vitambulisho walikuwa 200, lakini waliofanikiwa kuandikishwa ni 127.
“Hali ilivyo sasa ni tofauti na jana (juzi) kwani mtu mmoja kujiandikisha inachukua kati ya dakika sita hadi 10, wakati ilikuwa zaidi ya hapo, hii inatokana na ukweli kuwa watendaji wake wanaonekana wameshazizoea mashine,” alisema Tweve na kuongeza kuwa:
“Watu wanaokwenda kwenye vituo kujiandikisha idadi yao ni kubwa kuliko hata makadirio ya tume, kama hawataongeza muda au vifaa, siku saba walizopanga, hazitatosha na wengi wataachwa bila ya kujiandikisha,” alisema.
Baadhi ya waandikishaji na wasimamizi wa mashine wameiomba Tume ya Taifa ya Uchaguzi (Nec) kuongeza muda ili kazi hiyo ifanyike kwa ufanisi zaidi.
Hatua hiyo inatokana na kuharibika mara kwa mara kwa mashine hizo, wananchi kupigwa picha ambazo hazionekani kwenye kitambulisho, kukosewa tarehe na jina pamoja na alama za vidole kutokamilika kutokana na vidole kuwa na sugu .

Akizungumza katika kituo cha Mwembetogwa, opereta wa mashine ya kuchukua alama ya vidole na picha, Typhone Lumato alisema kazi inaendelea vizuri, licha ya mashine na kichapishi kuharibika mara kwa mara.
Alisema hali hiyo inasababisha usumbufu kwa wananchi ambao wapo kwenye foleni kwa muda mrefu kusubiri huduma hiyo.
Share on Google Plus

About Unknown

This is a short description in the author block about the author. You edit it by entering text in the "Biographical Info" field in the user admin panel.
    Blogger Comment
    Facebook Comment

0 comments:

Post a Comment