HOFU YATANDA: KADA WA CCM WAPATA WAKATI MGUMU KUMTAFUTA MRITHI WA RAIS JAKAYA KIKWETE!!

MCHUANO wa kumtafuta mrithi wa Rais Jakaya Kikwete, katika nafasi ya urais ndani ya chama kikongwe CCM umefikia hatua ngumu kutokana na kubadilika kwa upepo huku baadhi ya makada wake wakijipanga kuhamia upinzani endapo watakosa nafasi hiyo.

Hali hiyo imebadilika ikiwa imebaki siku moja kabla ya waziri mkuu aliyejiuzulu, Edward Lowassa,  kutangaza nia kugombea nafasi hiyo ya urais katika mkutano wake utakaofanyika mkoani Arusha, Jumamosi wiki hii.

Kwa sasa kuna taarifa kuwa ndani ya chama hicho hali imebadilika na kukifanya chama hicho kuwa katika nafasi ngumu.

Taarifa ambazo zimetufikia jana, zimeeleza kwamba makada hao wamefikia msimamo huo kutokana na kile wanachodai kuna dalili za chama hicho kufanya makosa katika uteuzi jina la mgombea, hali itakayowapa nafasi wapinzani kushinda kwa kishindo kwenye uchaguzi huo.

Mapema wiki hii baadhi ya vyombo vya habari vilinukuu makada wa CCM wakidokeza kwamba wana wasiwasi mkubwa kwa baadhi ya makada wake maarufu kuchukua hatua za kukihama chama hicho kama hawataridhishwa na mchakato mzima wa kupata jina la mgombea wa chama hicho.

Makada waliozungumza kwa sharti la kuhifadhiwa majina yao walitaja jina la mawaziri wawili mmoja akiwa waziri mstaafu na mwingine ni waziri katika Serikali ya Rais Kikwete na jina la mbunge mmoja ambaye aliwahi kuwa waziri katika serikali hiyo kwamba wanahofiwa kuchukua uamuzi huo mzito endapo hawataridhishwa na uteuzi wa jina la mgombea wa CCM.

Hata hivyo, inadaiwa kuwa baadhi ya makada wenye msimamo mkali wanatishwa na upepo unaovuma na kuonesha nguvu kubwa ya Lowassa ambaye anaonekana kuwa na nguvu kubwa miongoni mwa wagombea wa CCM, hali inayotishia kushinda uteuzi huo.

Pamoja na hali hiyo, baadhi ya makada ndani ya CCM wanaamini kwamba kiongozi huyo hatoshi kwenye nafasi hiyo hali inayoweza kutoa nafasi ya wazi wapinzani wanaounda kundi la UKAWA kushinda nafasi hiyo.

Chanzo chetu cha habari kilieleza kwamba makada hao wa CCM wanaohofiwa kujipanga wanaweza kukimbilia Ukawa kwa lengo moja tu la kusaka kuteuliwa kugombea nafasi hiyo ili wapambane na Lowassa kama atapitishwa na CCM kwa imani kwamba watakuwa na nafasi kubwa ya ushindi.

Mtoa habari wetu huyo alisema; "Makada wanaosaka urais CCM wanahofu kwamba Lowassa anaweza kuteuliwa kusimama kugombea urais kupitia CCM kutokana na mazingira na kauli za viongozi wa CCM zinazotolewa sasa.

Hali hiyo imefanya baadhi ya makada wanaoamini kwamba Lowassa hatoshi kwenye viatu vya urais kujipanga kwenda Ukawa ili kukabiliana naye endapo atapitishwa na CCM.”

Chanzo hicho kimesisitiza kwamba wanachama wengi ndani ya CCM wanaamini kwamba Lowassa anaweza kuibuka na ushindi mkubwa ndani ya vikao vya chama, lakini atakapokwenda kwa wananchi na kukutana na hoja za upinzani mbele ya umma zilizochangia kumng’oa uwaziri mkuu, atapoteza nafasi hiyo.

Kauli ya Mwenyekiti wa Chadema Freeman Mbowe aliyoitoa kwenye gazeti moja akidai kwamba Lowassa ni dhaifu na ‘bubu’ kutokana na kwamba hana ubavu wa kukemea rushwa, ufisadi  na ubadhirifu inawapa nguvu makada wa CCM wanaotaka kukimbilia Ukawa ili kukabiliana naye endapo atapitishwa na CCM.

Alisema makada wanaowania urais wanamjua vizuri sana hivyo wanaamini kwamba wakiachwa watakimbilia Ukawa na huko watakuwa na hoja za kutosha kupambana naye na nafasi yao ya ushindi itakuwa kubwa.

Wakati huo huo, huko mkoani Mbeya macho na masikio ya Watanzania yanatarajiwa kuelekezwa mkoani Mbeya Juni Mosi, mwaka huu wakati Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais (Kazi Maalum) Profesa Mark Mwandosya, atakapotangaza rasmi kuwania urais kurithi nafasi inayoachwa na Rais Jakaya Kikwete, ambaye anamaliza muda wake kwa mujibu wa Katiba.

Akizungumza kwa njia ya simu akiwa nchini Vietnam jana alikokwenda kumwakilisha rais, Prof. Mwandosya alisema kuwa siku hiyo (Jumamosi) atatangaza rasmi kuwania tena nafasi hiyo ambayo mwaka 2005 aliwania  na kufanikiwa kushika nafasi ya tatu.

Hatua hiyo bado inatafsiriwa kwamba wana-CCM wana imani kubwa na yeye, hivyo katika mchuano wa mwaka huu ana nafasi ya kufanya vizuri zaidi. Alisema kuwa  baada ya kuwa mbunge na waziri kwa kipindi cha miaka 15 akiwa anachaguliwa na wananchi wa  Busokelo mara zote bila  kupingwa  hali ambayo imempa nguvu wakati wote na kuona kuwa ni wakati wa kuachia nafasi hiyo na kumwachia  mwingine na kisha yeye kurudi ulingoni kwa ajili ya  kuomba ridhaa  na kuwaongoza Watanzania wote.

Prof. Mwandosya alisema kuwa yeye anajivunia kuwa mzalendo aliyesomeshwa kwa kodi za Watanzania na hivyo anaona deni la kuwatumikia Watanzania kwa uaminifu mkubwa kama ambavyo ameonesha wakati wote alioaminiwa na Rais Dkt.Jakaya Kikwete pamoja na Rais mstaafu, Benjamin Mkapa.

Alisema rekodi yake haina shaka inamsukumu awatumikie Watanzania. Waziri huyo  alisema ameamua kutoa heshima kubwa kwa wazazi wake wa Mkoa wa Mbeya kwa kuamua  kurudi nyumbani  kutangaza azima hiyo ambapo pia kwa kutambua kuwa yeye amekuwa akitumikia CCM  wakati wote ameona vyema kwenda makao makuu ya chama  hicho mkoani Mbeya kwa ajili ya kutangaza nia.

Wananachi wa Mkoa wa Mbeya  na mikoa  jirani wakizungumzia hali hiyo wamesema wamejipanga  kwa ajili ya kumpokea  kiongozi huyo. Walisema atapata mapokezi ya kishindo kikubwa.

Mzee Daimon Mwasampeta, ambaye  ni  kiongozi mstaafu wa chama cha NCCR-Mageuzi alisema Profesa Mwandosya ni mtu wa watu wote pasipo kujali itikadi na hivyo kinachotakiwa ni kuhakikisha anatumia uwanja wa Sokoine ili azungumze na Watanzania wengi bila kujali itikadi zao kama rais mtarajiwa.

Mwenyekiti mstaafu wa CCM Mbeya Mjini, Allan Mwaigaga, alisema Watanzania wanapaswa waache woga katika kipindi hiki cha kuelekea uchaguzi kwa kuhakikisha wanasema wazi kuwa  umefika wakati wa rais kutoka  katika mikoa ya Mbeya, Iringa  na Njombe kutokana  na ukweli kuwa haijawahi
kutoa rais wala waziri mkuu.

Mwaigaga ambaye ni mfanyabiashara mmiliki wa mabasi ya  Ndenjela,  alisema
kuwa Watanzania hususani wanaotoka katika mikoa hiyo iliyosahaulika wanapaswa kuweka msimamo mkali kwa kuwaunga mkono wagombea wao ili kuonesha usawa katika nchi ya Tanzania.

Alisema Mkoa wa Mara umetoa Rais, Arusha Waziri Mkuu, Pwani Rais, Katavi Waziri Mkuu, Dodoma  Waziri  Mkuu, Mtwara Rais na hivyo kuonesha wazi kuwa sasa  ni wakati wa mikoa  ya Mbeya,  Iringa na Njombe kutoa rais.

Share on Google Plus

About Unknown

This is a short description in the author block about the author. You edit it by entering text in the "Biographical Info" field in the user admin panel.
    Blogger Comment
    Facebook Comment

0 comments:

Post a Comment