SERIKALI YAWANYOOSHEA KIDOLE WABUNGE WAFANYABIASHARA...WADAIWA KUTETEA HOJA ZILIZO NA MASLAHI KWAO...!!

  

 
 
 
    SIKU chache baada ya Rais Jakaya Kikwete kuteua na kuapisha makatibu wakuu, naibu makatibu wakuu wapya na makatibu tawala wa mikoa, wamekutana kujadili vipaumbele vya Serikali na kupeana maelekezo.
Akizungumza katika mkutano huo jana, Katibu Mtendaji, Ofisi ya Rais Tume ya Mipango, Dk Philip Mpango, alielezea umuhimu wa Serikali kuwa macho na baadhi ya wabunge wafanyabiashara, ambao wamekuwa wakitetea hoja kwa maslahi binafsi.
Alitoa hadhari hiyo, huku akielezea kuwa katika mazingira ya sasa, mwingiliano wa majukumu kati ya ngazi za kiutendaji za Serikali na ngazi za kisiasa kama Bunge na Baraza la Mawaziri vimeongezeka.


Alitolea mfano wa Kamati ya Bajeti ya Bunge, ambayo alisema ina wajibu wa kubainisha vyanzo vya mapato, kazi ambayo zamani ilikuwa ikifanywa na Serikali.
Pia Kamati hiyo, ina wajibu wa kubainisha viwango vya kodi au tozo, viwango vya kukopa na ukomo wa bajeti kwa dhana ya kuisimamia Serikali.
Alitaka maofisa masuuli kusimamia hatua zote za mzunguko mpya wa bajeti katika maeneo yao: “Maofisa masuuli mtambue nyakati zimebadilika, Bunge la sasa ni tofauti na la siku za nyuma.
Ni muhimu maandalizi ya mipango na bajeti yafanyike kwa weledi na kuzingatia ratiba.” Ili utekelezaji wa miradi ya maendeleo uanze mapema, Dk Mpango alitaka maofisa hao wakamilishe mapema mipangokazi na mtiririko wa rasilimali fedha kwa ajili ya uchambuzi baada ya bajeti zao kupitishwa na Bunge.
Pia aliwataka kuzingatia sheria za fedha na kuepuka kufanya uhamisho wa fedha tofauti na ilivyoidhinishwa na Bunge, kwa kuwa hatua hizo zitaibua hoja za Mkaguzi na Mdhibiti wa Hesabu za Serikali (CAG).
Aliwataka kupitia kwa umakini na kuhakiki takwimu na taarifa zote za utekelezaji wa bajeti na miradi ya maendeleo wanayoisimamia, kabla ya kuziwasilisha katika ngazi za kisiasa, likiwamo Baraza la Mawaziri na Bunge.
Akifungua mkutano huo wa siku tatu, Katibu Mkuu Kiongozi, Balozi Ombeni Sefue, alitaka washiriki kusimamia vipaumbele vya Taifa, vya Mpango wa Matokeo Makubwa Sasa, Serikali ya Wazi na Serikali mtandao.
“Ili kufanikisha mabadiliko, tunahitaji uongozi imara unaoweza kuandaa dira na mikakati inayotekelezeka, kuanzisha na kusimamia mageuzi na kuwasiliana. Kiongozi asiyeweza kuongoza mageuzi si kiongozi bora.
“Dunia inabadilika, nchi yetu inabadilika, matarajio ya wananchi kwa Serikali yanabadilika, hivyo ni lazima tubadili namna tunavyohudumia wananchi, kwani kuna watu wenye mitazamo au fikra finyu wanaoshuku madhumuni ya kila mabadiliko,” alisema.
Balozi Sefue alisema kwa sasa kuna changamoto za utendaji katika sekta ya umma, ambazo ni udhaifu katika ukusanyaji wa mapato na kufanya Serikali ishindwe kujigharimia kikamilifu pamoja na kuwepo malalamiko ya wananchi dhidi ya Serikali.
Alisema changamoto nyingine ni matumizi ya fedha za umma, ambayo hayaendani na thamani ya fedha na udhaifu katika kusimamia sheria, kanuni na taratibu.

Share on Google Plus

About Unknown

This is a short description in the author block about the author. You edit it by entering text in the "Biographical Info" field in the user admin panel.
    Blogger Comment
    Facebook Comment

0 comments:

Post a Comment