
KASHFA ya
 kumbaka na kutishia kumuua msichana wa miaka 16 inayomkabili Mbunge wa 
Urambo Magharibi, Profesa Juma Kapuya (CCM), imezidi kuchukua sura mpya 
baada ya serikali kutoa kauli nzito ya kutaka kumfungulia mashitaka 
mbunge huyo, Tanzania Daima Jumapili limebaini.
Mashitaka
 yanayotajwa kumkabili mbunge huyo ambaye amepata kuwa waziri katika 
awamu tofauti za uongozi, ni pamoja na ubakaji na kutishia kuua.
Kamishna 
wa Polisi Kanda Maalumu ya Dar es Salaam, Suleiman Kova, aliliambia 
gazeti hili jana kuwa jeshi hilo halitakuwa na sababu ya kumuacha mbunge
 huyo kuendelea kutamba mitaani huku akituma ujumbe wa vitisho kwa binti
 wa miaka 16 anayedaiwa kumbaka.
Alisema 
watachukua hatua za haraka kama mtoto huyo atakwenda kufungua jalada la 
kutishiwa maisha katika kituo chochote cha polisi jijini Dar es Salaam 
wakati wowote.
Kamishna 
Kova alisema hadi jana jeshi lake lilikuwa halijapata malalamiko yoyote 
kutoka kwa binti anayedai kubakwa na kutishiwa maisha na Profesa Kapuya,
 kupitia ujumbe mfupi wa simu ya mkononi iliyosajiliwa kwa jina la 
Profesa Kapuya na kuongeza kuwa muda wowote taarifa hizo 
zitakapofikishwa polisi wataanza kuzifanyia kazi.
"Sisi 
Polisi hatuna shamba hapa mjini zaidi ya kukabiliana na uhalifu... na 
huyo binti mwambie aje afungue malalamiko yake, tena amuone RPC yeyote 
katika mikoa ya kipolisi ya Dar es Salaam na si hili la kutishiwa tu, 
hata hilo analosema la kubakwa na sisi tutamuwajibisha aliyefanya hivyo 
katika makosa mawili tofauti," alisema Kamishna Kova.
Wakati 
Kamanda Kova akisema hawatakuwa na ajizi na tuhuma za kubaka na kutishia
 kuua zinazomkabili Profesa Kapuya, habari kutoka Ikulu ya Rais Jakaya 
Kikwete zinaeleza kuwa kiongozi huyo wa nchi amekerwa na kauli ya Mbunge
 huyo wa Urambo Magharibi kuwa serikali haiwezi kumfanya jambo lolote.
Ni 
kutokana na kauli hiyo mtoa taarifa wetu alisema rais aliagiza vyombo 
vya dola kufuatilia kwa karibu sakata hilo na kuhakikisha sheria 
inachukua mkondo wake.
Juzi 
gazeti hili lilinukuu moja ya ujumbe mfupi wa maneno kutoka katika simu 
ya Profesa Kapuya kwenda kwa binti anayedai kubakwa na Kapuya, sehemu ya
 ujumbe huo unasomeka kuwa: "Mkiuawa itakuwa vizuri....itawapunguzia 
gharama za kuishi, usitake kugombana na serikali mtoto mdogo kama wewe, 
sisi ndiyo wenye nchi yetu, mwenye hilo gazeti ni Mbowe, sasa mwambieni 
nyumba ya kuishi si mmemuingizia hela leo? Mnatumika tu bure watu 
wanaingiza hela nyingi, ila mmenitibua lazima niwaue wiki hii haitaisha 
nitapiga kambi kote, jana si wamekuficha, tuone utalindwa milele, maana 
washatengeneza hela lazima mvae sanda tu, hilo sio ombi ni wajibu wenu, 
mnajitia na nyie mafia watoto siyo, watoto wetu wanauza unga nani 
anawakamata? Nani atapingana nasi."
Pia kwa 
upande wa Chama Cha Mapinduzi (CCM), taarifa zinaeleza kuwa chama hicho 
kimeamua kumtosa mbunge huyo aliyewahi kuongoza Wizara ya Elimu na 
Ulinzi kwa nyakati tofauti baada ya kumtaka aache kukihusisha chama na 
kashfa yake ya kubaka.
Mmoja wa 
viongozi wa CCM aliyezungumza na gazeti hili kwa sharti la kutotaja jina
 lake kwa vile siye msemaji wa chama, alidokeza kuwa chama hicho 
kilijaribu kulimaliza suala hilo kimya kimya, lakini lilikwamishwa na 
Profesa Kapuya mwenyewe kwa kutofika kwenye vikao vya usuluhishi na 
binti huyo.
Pia imebainika kuwa baadhi ya wabunge waliokuwa wanataka kumsitiri Profesa Kapuya aliishia kuwaona kama wabaya wake.
"Hapa 
palipofika ahangaike peke yake, watu walijitahidi kadiri walivyoweza 
hili suala limalizike lakini mwenzetu alikuwa mzito kushirikiana nasi, 
sasa hakuna anayetaka chama kichafuke zaidi, amesubiriwa Dodoma na 
watoto wiki mbili hatokei, hadi watoto wakashauriwa kwenda kuwaona 
viongozi wakuu Dar es Salaam," alisema kiongozi huyo.
Juzi 
gazeti hili lilichapisha habari kuhusu mwanafunzi huyo aliyesema kuwa 
waziri huyo alimbaka kwenye hoteli moja ya kitalii iliyoko jijini Dar es
 Salaam mwaka 2011, na kurudia tena kitendo ndani ya ofisi yake katika 
Jengo la Biashara Complex lililoko Mwananyamala Juni 3, 2012 alipoitwa 
kwenda kuchukua ada kwa mara ya pili.
Kutokana 
na habari hiyo Profesa Kapuya kupitia kwa wakili wake, Yasin Memba, 
alitishia kuliburuza gazeti hili mahakamani endapo halitamwomba msamaha 
ndani ya siku saba.
Mbali na 
kutishia kulipeleka gazeti hili na baadhi ya mitandao ya kijamii 
mahakamani pia Profesa Kapuya alikana kumfahamu binti anayedai alibakwa 
huku akikanusha kumiliki simu namba 0784993930 ambayo imekuwa ikitumiwa 
kuwasiliana naye ikiwemo kumtumia ujumbe mfupi wa maneno (sms) wa 
vitisho.
Uchunguzi
 wa gazeti hili umebaini kuwa ni kinyume cha sheria za Mamlaka ya 
Mawasiliano nchini mtu kugawa namba iliyosajiliwa kwa jina lake.
Katika 
namna ya kushangaza, juzi Kapuya kupitia kwa wakili wake alidai kwamba 
simu hiyo aliishaigawa miezi sita iliyopita, hivyo hahusiki kwa namna 
moja ama nyingine na tuhuma alizopewa.
Wakati 
Kapuya akikana kumiliki simu hiyo, Novemba 9, mwaka huu gazeti hili 
liliwasiliana naye kupitia namba hiyohiyo anayodai kwamba alishaigawa 
miezi sita iliyopita.
Tarehe 
hiyo, gazeti hili liliwasiliana na mbunge huyo ili kuthibitisha tuhuma 
zilizokuwa zikimkabili wilayani Kaliua za kumpiga makofi kiongozi mmoja 
wa CCM.
Kapuya kupitia namba hiyo, alitoa utetezi wake ambapo gazeti hili lina sauti yake.
Utetezi 
wa Kapuya pia unaongeza utata kwa kushindwa kufafanua namna alivyoweza 
kugawa namba ya simu iliyosajiliwa kwa jina lake kwa mtu mwingine, huku 
ikiendelea kutuma fedha na vitisho kwa binti huyo.
Alilishutumu
 gazeti hili kuwa lilimhukumu na kuchapisha tuhuma zake bila kumpa 
nafasi ya kujitetea kama inavyoelekezwa katika tasnia ya habari.
"Kwa 
sababu hiyo, amenielekeza niwapatie siku saba gazeti la Tanzania Daima, 
mitandao ya kijamii ukiwemo wa Jamii Forum, Justina John na Vituko 
Mtaani, ambao walichapisha habari hiyo, waombe radhi kwa uzito uleule la
 sivyo atavishitaki mahakamani," alisema Memba wakati akizungumza na 
waandishi wa habari juzi.
CHANZO TANZANIA DAIMA.
POSTED BY:www.info@dirayetu.blogspot.com 
0 comments:
Post a Comment