MBOWE AZUA TAHARUKI DAR!!


 

JESHI la Polisi Kanda Maalumu ya Dar es Salaam, jana liliimarisha ulinzi ndani na nje kwenye majengo ya Makao Makuu ya Jeshi hilo na kusababisha taharuki kubwa kwa wapita njia baada ya Mwenyekiti wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA), Bw. Freeman Mbowe, kuwasili katika ofisi hizo.

Bw. Mbowe alifika katika ofisi hizo saa tano asubuhi kwa ajili ya mahojiano akidaiwa kutoa kauli ya kuitisha maandamano yasiyo na kikomo nchi nzima ili kushinikiza Bunge Maalumu la Katiba lisitishe vikao vyake kabla ya Oktoba 4 mwaka huu.

Nje ya ofisi hizo, kulikuwa na askari wenye mbwa, gari la maji ya kuwasha, askari waliokuwa na sare za jeshi wakiwa na silaha za moto na waliovaa kiraia ambao walionekana wakiranda maeneo yote ya Posta Mpya.

Gari ya Bw. Mbowe ilipofika lango kuu la kuingilia katika ofisi hizo, lilizuiliwa na polisi ambao walimtaka ashuke na kuingia ndani peke yake bila gari lakini wafuasi wake waliokuwa nje, walianza kupiga kelele wakitaka aruhusiwe kuingia na gari.

Wafuasi hao walisikika wakiimba "People's Power...People's Power" na wengine wakisema "Rais ajaye, Rais ajaye...amewasili Makao Makuu ya Polisi".

Mzozo huo ulidumu kwa dakika 10 ndipo akaruhusiwa kuingia nagari lake ambapo muda mchache baadaye, aliwasili Mwanasheria wa CHADEMA, Bw. Tundu Lissu akiwa kwa miguu akazuiliwa kuingia ambapo mzozo huo ulidumu kwa robo saa akaruhusiwa.

Wengine waliozuiliwa kuingia katika ofisi za Makao Makuu ya jeshi hilo ni Mbunge wa Kawe, Bi. Halima Mdee, Mbunge wa Nyamagana, mkoani Mwanza, Bw. Ezekiah Wenje na Bw. Joseph Mbilinyi mbunge wa Mbeya Mjini baada ya kufika katika ofisi hizo kwa kuchelewa.

Wafuasi wa chama hicho walionekana wakiranda katika maeneo mbalimbali ya Posta Mpya baada ya kutimuliwa nje ya geti la Makao Makuu ya Polisi.

Baadhi ya wananchi waliofika Posta Mpya kwa shughuli mbalimbali, waliingiwa na hofu ya kupigwa mabomu ya machozi kama zitatokea vurugu kati ya polisi na wafuasi wa CHADEMA ambapo baadhi ya watu waliofika Makao Mkuu ya jeshi hilo kwa mahitaji ya kiofisi, walilazimika kuondoka.

Kauli ya John Mnyika

Ilipofika saa saba mchana, Mbunge wa Ubungo, Bw. John Mnyika, alitoka nje ya ofisi za jeshi hilo ili kuzungumza na wafuasi wa chama hicho akiwataka wawe watulivu wakati Mbowe akiendelea kuhojiwa.

"Baada ya kuingia ndani, Mbowe alioneshwa mkanda wa video waliodai alitoa kauli za uchochezi zenye kuhamasisha vurugu katika mikutano...muda wote alikuwa hajaanza kuhojiwa kwa sababu kulikuwa na ubishani baada ya kuoneshwa mkanda.

"Mbowe alitakiwa kutoa maelezo kwa kuandika barua ya kukiri yeye ni mchochezi lakini alikataa, badala yake alikubali kuandika barua yenye maelezo kuwa kwanini amekataa," alisema.

Baada ya masaa mawili, Bw. Lissu, alitoka nje ya ofisi hizo baada ya mahojiano kumalizika na kusema kuwa, Bw. Mbowe amepewa dhamana ambayo ilikuwa ikishughulikiwa na Bi. Mdee na kiongozi mwingine wa CHADEMA hivyo aliwataka wafuasi wa chama hicho watawanyike kwani wakikaidi, polisi watatumia nguvu.

"Kilichoafikiwa ni kwamba, Mbowe atasindikizwa na moja ya magari ya polisi hivyo nawaomba muondoke eneo hili muende katika ofisi za chama au nyumbani bila kufanya maandamano yoyote hadi mtakapotangaziwa," alisema Bw. Lissu.

Share on Google Plus

About Unknown

This is a short description in the author block about the author. You edit it by entering text in the "Biographical Info" field in the user admin panel.
    Blogger Comment
    Facebook Comment

0 comments:

Post a Comment